25 November 2010

Zantel kudhamini mashindano ya gofu.

Na Amina Athumani

KAMPUNI ya simu za mkononi Zantel, jana imetangaza udhamini wa mashindano ya gofu ya mwisho wa  mwezi yatakayofanyika Jumamosi katika viwanja vya Gymkhana, Dar es Salaam.
Akitangaza udhamini huo Dar es Salaam jana, Ofisa Mkuu wa Masoko wa Zantel Nitish Malik, alisema kampuni yake imeamua kudhamini mashindano hayo, ili kusaidia kuukuza mchezo huo uweze kupiga hatua na kufahamika zaidi kwa Watanzania.

"Gofu ni moja ya mchezo maarufu sana duniani kwa hiyo ninaimani udhamini huu wa Zantel, katika mashindano haya utazidi kuutangaza mchezo huu zaidi nchini na wengi watajitokeza zaidi kuucheza na kuufahamu," alisema Malik.

Alisema mwendelezo wa udhamini kwa Zantel, katika mchezo wa gofu utakuwa changamoto kwa watu wengine kujifunza gofu na pia kuweka uwezekano wa kupata wachezaji wazuri ambao baadaye wataweza kuiwakilisha nchi katika michezo ya kimataifa na kuitangaza Tanzania vyema kimataifa.

Naye nahodha wa Klabu ya Gymkhana, Joseph Tango aliishukuru Zantel kwa kudhamini mashindano hayo kwa kuunga mkono juhudi za maendeleio ya michezo nchini na kuwataka wanamichezo kutumia fursa hiyo kujitokeza na kushiriki kwa wingi michuano hiyo.

No comments:

Post a Comment