27 August 2012

Wavuvi waokolewa Z'bar, mmoja afariki dunia



Na Mohammed Mhina, Jeshi la Polisi Zanzibar

WAVUVI wawili raia wa nchi jirani ya Komoro, wameokolewa kwenye kisiwa kidogo cha Pungume, nje kidogo ya Zanzibar wakiwa hoi kutokana na uchovu, njaa baada ya kupotea baharini siku 11 bila kula chakula wakiwa na boti ndogo ambayo iliishiwa mafuta.

Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi Zanzibar, Kamishna Msaidizi (ACP), Yusufu Ilembo, amewataja wavuvi hao kuwa ni Othman Inzudin (24) na Bw. Nurdin Ahmed (18).

Alisema wavuvi hao wakiwa katika shughuli za uvuvi nchini Komoro, walipatwa na mtikisiko wa mawimbi, upepo mkali na kupotea baharini hadi boti yao ilipoishiwa mafuta.

Aliongeza kuwa, kutokana na hali hiyo vijana hao walijikuta wakiishi majini muda mrefu bila chakula, kunywa maji ya chumvi wakati boti yao ikifuata mwelekeo wa mawimbi na upepo hadi walipofika Kisiwa cha Pungume, Kusini mwa Zanzibar.

“Hawa vijana walilazimika kufungua injini ya boti yao na kuitosa majini kama njia ya kufanya iwe nyepesi ili isukumwe na mawimbi kwa urahisi na kufika nchi kavu kunusuru maisha yao,” alisema.

Kamanda Ilembo aliongeza kuwa, baada ya vijana hao kuokolewa, walipelekwa katika Hospitali Kuu ya Mnazimmoja kwa matibabu lakini baada ya muda mfupi, Ahmed alipoteza maisha wakati madaktari wakiendelea kuokoa maisha yake.

Alisema Jeshi la Polisi limewasiliana na Ubalozi wa Komoro nchini ili kuangalia uwezekano wa kumsafirisha mvuvi mmoja aliyebaki pamoja na mwili wa marehemu ili aweze kwenda kuzikwa huko.

Wakizungumza na Majira, baadhi ya madaktari na wauguzi wa zamu katika hospitali hiyo, Dkt. Mohammed Hassan Haji na Dkt. Mkasi Khatib Makame, walisema saababu ilichongania kifo cha Ahmed ni uchovu, njaa na hali ya kukata tamaa kutokana na wasiwasi.

Walisema hali ya mvuvi aliyebaki wodini inaendelea vizuri baada ya kuongezewa maji mwilini na kupewa chakula ambacho kimesaidia kumpa nguvu zaidi.

No comments:

Post a Comment