07 December 2010

Nahodha asisitiza ulinzi shirikishi

Na Eckland Mwaffisi

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Bw. Shamsi Vuai Nahodha amesema kipaumbele cha Wizara hiyo kwa sasa ni kuimarisha dhana ya ulinzi shirikishi ili wananchi waweze kushiriki kikamilifu katika masuala la ulinzi na usalama wa mali zao.Bw. Nahodha aliyasema
hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na viongozi wa Jeshi la Polisi Makao Makuu na Kanda ya Dar es Salaam, katika kikao chake cha kwanza na viongozi hao baada ya kuteuliwa katika nafasi hiyo hivi karibuni.

Alisema wananchi wengi wameonesha nia ya kushirikiana na Jeshi la Polisi katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu ila baadhi yao, wanakatishwa tamaa na ushirikiano hafifu unaotolewa na baadhi ya watendaji wa jeshi ambao hupokea taarifa zao na kuzitumia vibaya.

Aliwataka viongozi wa jeshi hilo kujipanga upya na kuweka mikakati ambayo itaboresha ushirikiano na wananchi ili kukabiliana na vitendo vya uhalifu ambavyo bado ni tishio kwa usalama wa raia na mali zao.

“Jeshi la Polisi peke yake haliwezi kukabiliana na vitendo vya uhalifu, njia pekee ambayo itawezesha kudhibiti vitendo hivi ni kushirikina na wananchi,” alisema Bw. Nahodha na kuwataka viongozi hao, kuhakikisha kuwa taarifa zinazotolewa na wananchi, zinatumiwa kwa malengo yaliyokusudiwa.

Katika kikao hicho, Bw. Nahodha ametaja vipaumbele vingine kuwa ni kusimamia maboresho ya jeshi hilo ili liweze kutoa huduma bora kwa wananchi.
“Serikali kwa upande wake, itafanya kila linalowezekana kuhakikisha maslahi ya askari yanaboreshwa ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi,” alisema.

Leo Bw. Nahodha atakuwa na mkutano na askari polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam.

1 comment:

  1. Mheshimiwa Nahodha,pamoja na juhudi zako zenye nia nzuri.Ninaomba sana uwakumbuke wafungwa weye vifungo vya maisha hususani walioka gerezani zaidi ya miaka 10 na kuendelea.Kwa jinsi ninavyoelewa waziri wa mambo ya ndani huwa ndie katibu kikao cha msamaha kwa wafungwa.Lakini cha kushangaza wafungwa wa kifungo cha maisha huwa hawapewi msamaha kwa nchi ya Tanzania.

    ReplyDelete