07 November 2010

CCM Arusha yazuia vijana wake kuandamana.

Na Queen Lema, Arusha

UONGOZI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Arusha umepinga na kulaani maandamano
yanayodaiwa kupangwa na baadhi ya vijana wa
CCM yakupinga  matokeo ya ubunge wa Jimbo la Arusha
lililochukuliwa na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wakitaka viongozi wa Wilaya CCM wajiuzulu kwa madai ya  kuuza jimbo kwa chama cha upinzani.

Akizungumza na  Majira Jumapili,  Katibu wa CCM  Mkoa wa Arusha Bi. Mary Chatande alisema kuwa uongozi wa CCM haukuwa na taarifa ya maandamano hayo na kuwa chama hicho kimekubaliana na matokeo na kusisitiza kuwa mgombea ama wakereketwa wa chama hicho ambao  hawakuridhika na matokeo waende mahakamani .

Bi. Chatande alisema kuwa Mratibu wa Uchaguzi CCM, Taifa ametoa tamko  kuhusu taratibu za kutafuta haki na kuwa mgombea akienda mahakamani atapewa ushirikiano na chama na siyo kuhamasisha maandamano kinyume na taratibu ambayo  yanaweza kusababisha uvunjwaji wa amani

Akifafanunua zaidi alisema kuwa hakuna ushahidi kuwa jimbo
hilo limeuzwa na vingozi kama wanavyodai baadhi ya vijana na wapambe wa mgombea na kuwa kama kuna madai hayo ni vyema yapelekwe mahakamani.

 "Wananchi wanapaswa kujua na kutambua kuwa sisi hatujauza hili jimbo kwa CHADEMA kama wanavyosema baabdhi ya wakazi wa jimbo la arusha  mjini, "alisema Bi Chatande.

Bi Chatande alieelezea sababu mojawapo ambayo imesababisha jimbo hilo kuchukuliwa na CHADEMA kuwa ni pamoja na ushirikiano finyu baina ya kamati ya siasa na mgombea Dk.Batlida Burian.

“Kulikuwa na taarifa kuwa mgombea hakuwa tayari kuvunja
makundi yaliyokuwa yamejitokeza katika kura za maoni na hivyo kusababisha hali hiyo kumpa ushindi mgombea wa upinzani," alisema Bi. Chatande.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Bassilio Matei aliwaambia waandishi wa habari kuwa maandamano  hayo ni batili na hakuna maandamano yanayoruhusiwa hadi Rais aapishwe.

No comments:

Post a Comment