16 December 2011

Msitegemee ajira serikalini pekee-Kabaka

Na Nickson Mahundi

SERIKALI imewataka vijana nchini kuacha kasumba ya kusubiri ajira serikalini badala yake watafute njia ya kujiari wenyewe katika shughuli mbalimbali za uzalishaji.Ushauri
huo ulitolewa Dar es Salaam jana na Waziri wa Kazi na Ajira Bi.Gaudencia Kabaka, wakati wa mahafali ya Vijana wa Kazi nje nje(KNN) na mashindano ya mpango wa wazo la biashara kitaifa linaloendeshwa na Shirika la Kazi Duniani (ILO).

ILO ilibuni mpango wa KNN nchini kwa lengo la kuwawezesha vijana kubuni miradi mbalimbali nya maendeleo na kufuta dhana ya kukaa kusubiri ajira serikali baada ya kuhitimu masomo katika viwango mbalimbali.

Waziri Kabaka alisema serikali inatoa ajira kwa asilimia tatu tu kwa vijana lakini imeandaa mazingira mazuri yanayowawezesha kujiajiri na kuwaajiri wengine.

Alisema mpango huo wa KNN unaoendeshwa na ILO kwa kushirikiana na Wizara yake ina umuhimu mkubwa kwa vijana wa Kitanzania kwa kuwawezesha kuondokana na umasikini hivyo kuwataka kuutilia mkazo na kuwa waaminifu katika miradi watakayoanzisha.

"Serikali sio mwajiri pekee nchini, ni watanzania wachache wanaopata ajira, pia kuna wadau wengi wanaoweza kuajiri lakini kinachofanywa na serikali ni kuandaa mazingira mazuri yatakayowawezesha vijana kujiajiri na kuwaajiri wengine,"alisema Bi. Kabaka.

Bi. Kabaka aliongeza kuwa Mtanzania yeyote mwenye uwezo wa kuandaa mpango utakaoongeza ajira anakaribishwa na kwamba iwapo atahitaji msaada kuboresha mpango wake atahudumiwa ipasavyo.

Akizungumza kwa niaba ya wajasiriamali wa makundi maalumu Bw. Daudi Mpalahingwe, alisema mafunzo hayo yatawawezesha kufikisha elimu hiyo kwa wengine na kuwaajiri vijana wengine.

Bw. Kapalahingwe alisema mafunzo ya ujasiriamali ni nyenzo muhimu katika kujikwamua na umaskini hivyo kuwaomba viongozi wa mradi huo kuyafikia makundi maalumu yaliyoko vijijini ili kuyawezesha kujitengemea katika uzalishaji.

Mahafali hayo yaliambatana na ugawaji vyeti kwa wahitimu wa KNN pamoja na zawadi za fedha taslimu kwa washindani wa mpango wa wazo la biashara kitaifa ambao walitoka mikoa 12 nchini.

1 comment:

  1. Serikali inatatakiwa kuandaa fursa ambazo zinaweza kufanya Mtanzania aweze kujiari, leo hii una maliza chuo chochote kile hata kama umepata ujuzi wako wa kuweza kujiajiri bado utakumbana na vikwazo vingi sana hasa katika swala la kuweza kupata mkopo wa kuweza kujianzishia biashara yako maana taasisi za fedha zina mashariti magumu ya kupata mkopo. Kama serikali wangekuwa makini hawa wote wanao maliza kozi mbalimbali ingeweza kuweka sera ya kuwasaidia waweze kupata hiyo mkopo kwa riba nafuu na ipatikane kwa urahisi serikali ikiwa ndiyo wadhamini wakuu.Sasa hapo hata kama hawa viongozi wangewambia watu jamani mstitegemee ajira toka serikalini maana tayari imesha andaa mazingira mazuri ya watu wake kuweza kuji ajiri.

    ReplyDelete