20 July 2011

SAKATA LA RUSHWA

Ngeleja, Malima nao wakabwa koo

*Katibu Mkuu mstaafu ataka wawajibishwe haraka
*Lema amwandama Jairo bungeni, Makinda amtetea


Na Tumaini Makene

SIKU moja baada ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kuonesha kusikitishwa na kitendo cha Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Bw. David Jairo kuagiza idara za
wizara hiyo kuchangia gharama za kukamilisha maandalizi na uwasilishaji wa bajeti, Katibu Mkuu Mstaafu katika wizara mbalimbali, Bw. Nerei Msimbira, amesema alitegemea serikali ingechukua hatua mara moja, ikibidi hata siku hiyo hiyo.

Akizungumza na gazeti hili wakati wa mahojiano maalum Dar es Salaam jana, Bw. Msimbira, ambaye aliwahi kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji, Ardhi na Habari na Utangazaji alisema aibu hiyo si Bw. Jairo, pekee yake, bali ni aibu ya mfumo mzima.

Alisema hivyo akionesha mashaka iwapo hatua stahili zitachukuliwa akikumbushia namna ambavyo watuhumiwa wa kashfa ya Richmond walivyoachwa, wengine wakastaafu na wengine kupandishwa vyeo, hata baada ya kuwepo maazimio ya bunge kuwa wachukuliwe hatua.

Alizidi kusema kuwa; "Jambo hilo ni kubwa na
'aibu na hatari." Alisema vitendo vya namna hiyo vilisababisha kufa kwa mashirika mengi ya serikali.

Aliongeza kuwa inashangaza kuona suala 'kubwa' kama hilo la idara 21 ya serikali kuombwa kiasi
cha sh. milioni 50 kila moja, linaweza kufanywa na mtu mmoja, bila mfumo wa wizara au serikali kushiriki au kujua mapema.

"Hili suala si la kimaadili. Kama wana ushahidi wangechukua hatua mara moja hapo hapo. Vitendo kama hivi ndivyo viliua mashirika ya umma huko nyuma. Mtu
unakwenda Dodoma kisha unaanza kuagiza fulani leteni milioni mia moja hapa, sasa wakati huo serikali wanataka na chama nacho kinataka.

"Unajua labda kama ni milioni moja sawa, lakini milioni 50, sasa watafanyaje kazi, kwanza si unakuwa umeshauwa hiyo idara sasa. Sasa na bajeti haikupita na hizo fedha tayari zimekwenda itakuwaje...maana hili jambo lilianza anza hapo nyuma kidogo, sijui
kuna pesa zimetolewa kushawishi hivi na vile.... lakini haliwezi kuwa la mtu mmoja hili, hizo ni fedha nyingi, milioni hamsini mara ngapi sijui, nimesoma idara 21  yaliombwa," alisema, Bw. Msimbira na kuongeza;

"Ni suala la ajabu hivi, that is hopeless, tena unaandika kabisa na unasaini, unawaamini vipi au unamwamini vipi kila anayelipitia faili hilo. Hivi si ndiyo namna hawa watu wa upinzani, akina CHADEMA wanapata siri hizo wanazozitoa, unafikiri wanapataje...I mean...yaani mtu anawezaje kufanya hivyo bila system nzima kuwa inajua...huwezi kufanya namna hiyo, hizo ni bilioni za fedha, kwanza hata waziri tu lazima angemuuliza.

Katibu Mkuu huyo mstaafu ambaye kwa sasa anajishughulisha na kazi zake binafsi za utaalam wa kushauri masuala ya uhandisi na mipango, alionekana kusita kukubali kuwa suala hilo halikuwa likijulikana kwa wakubwa wengine wa Bw. Jairo, akisema 'hiyo haiwezekani, haiwezi kuwa serikali hiyo labda kitu kingine kabisa, labda ungekuwa unaongelea milioni moja, lakini milioni hamsini mara ishirini na moja, aah".

RUSHWA YAKERA UPINZANI

Naye Peter Mwenda anaripoti kuwa watu mbalimbali waliozungumza na gazeti hili Dar es Salaam jana walisema kilichobaki ni viongozi wa wizara ya Nishati na Madini kuachia ngazi.

Mhadhiri wa Kitivo cha Sheria Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Dkt. Sengondo Mvungi, alisema kwa sasa Bunge limeelewa kazi yake, kwa vile limeanza kujua thamani na heshima wanayostahili kuwa nayo Watanzania.

Alisema kwa mara ya kwanza wabunge wamezungumza kwa majonzi na uchungu mkubwa wa hali waliyonayo watanzania na kuongeza kuwa Bunge kama lingekuwa na msimamo kama huu siku zote, Tanzania ingepiga hatua kubwa ya maendeleo.

"Tangu awamu ya tatu tulizungumzia paka asiyekamata panya ambayo ni Kampuni ya Net Group Solution, haikuja na kipuri wala senti moja lakini walichota fedha zetu wakaondoka, tatizo la umeme lilianza kuonekana kuwa kubwa tangu serikali ya awamu ya tatu, "alisema Dkt. Mvungi.

Alisema ili kufikia malengo ya milenia, Tanzania inatakiwa kuzalisha megawati 6,000 mpaka megawati 7,000 kutokana na utajiri wa gesi iliyopo nchini.

"Mitambo iliyonunuliwa kwa ajili ya kufunga Dar es Salaam kwanini isiende kufungwa Songosongo inapotoka gesi,hiyo ni akili ya kizembe kwa tatizo kubwa la umeme kama hili, "alisema Dkt. Mvungi.

Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, Bw. James Mbatia alisema hatua iliyofikiwa na Bunge imetokana na uzembe wa viongozi wa Serikali ya CCM.

Alisema tatizo la mahitaji makubwa ya umeme ni la muda mrefu kutoka miaka ya 1980 wakati wa utawala wa Mwalimu Julius Nyerere lakini halikufanyiwa kazi kitaalamu.

Alidai kuwa bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini ni chafu, iliyojaa makosa mengi ambayo haistahili kupitishwa kwa maslahi ya watanzania.

Alisema kama Serikali ingekuwa makini hata kuvuna maji ya kutosha kipindi cha masika kwa ajili ya kuzalisha umeme ungefanikiwa kuzalisha umeme wa kutosha.

Alisema Tanzania inayo gesi ya kuzalisha umeme wa kutosha na kuuza nchi nyingine za jirani,kuzalisha umeme kutumia makaa ya mawe lakini tatizo kuwa wataalamu hawapewi nafasi ya kuonesha uwezo wao.

Mwenyekiti wa APPT Maendeleo Bw. Peter Mziray, alisema kabla ya Bunge hili wabunge waliokuwepo walikuwa wakipitisha hoja hata kama inawaumiza watanzania.

Alisema kitendo cha Katibu Mkuu Bw, Jairo kutaka taasisi za wizaya hiyo kuchangia sh. mil. 50 kwa ajili ya kutoa hongo kwa wabunge ni kosa ambalo TAKUKURU inatakiwa imkamate na kumfungulia mashtaka haraka.

Alisema hiyo ni aibu kwa watanzania kwa sababu Baraza la Mawaziri na watendaji wao ni jipya na waliaminika lakini kutokana na kasoro hizo ni feki hivyo livunjwe.

Bw. Mziray alitaka Waziri Ngeleja na Katibu wake Mkuu Bw. Jairo wajing'atue madarakani haraka kabla ya Rais Kikwete kurejea nchini.

Alisema wakati Serikali inatafakari kutafuta njia mbadala ya mgawo wa umeme waingize vifaa vya umeme wa jua yaani sola bila kutoza ushuru ili angalau baadhi ya huduma ambazo hazihitaji umeme mwingi ziendelee.

Alisema kutokana na hali tete ya upatikanaji wa umeme vifaa vya sola vinaweza kusaidia kutumika kama vibatari ili kupata mwanga wa kufanya shughuli nyingine ndogondogo ziendelee.

Alisema kutokana na hali hiyo kufikia hali ngumu ya kuendelesha maisha ya kila siku ya wananchi siku ambayo watanzania wakiamua kufanya maandamano ya mgawo wa umeme ndiyo siku ambayo Rais Kikwete ataachia madaraka.

MBUNGE ATAKA NGELEJA, MALIMA WAWAJIBISHWE

Gladness Mboma anaripoti kutoka Dodoma kuwa Mbunge wa Arusha Mjini, (CHADEMA), Bw.Godbless Lema amehoji bungeni ni kwa nini Bw. David Jairo anayehusishwa na vitendo vya rushwa katika upitishwaji wa bajeti ya wizara hiyo, awajibishwe peke yake wakati mawaziri nao wanaonekana kuhusika na taarifa hiyo.
 
Alisema katika suala hilo, Waziri wa Nishati na Madini, Bw. William Ngeleja na naibu wake,Bw. Adam Malima wanapaswa kuwajibishwa kwa kuwa si rahisi maamuzi hayo kuyatoa Katibu Mkuu peke yake.
 
“Naomba mwongozo wako mheshimiwa Spika inawezekanaje Katibu Mkuu kupitisha suala hilo bila ya waziri na naibu wake kujua. Je anayepaswa kuwajibishwa ni Katibu Mkuu peke yake,” alihoji. Hata hivyo, Spika wa Bunge, Bibi.Anne Makinda, alisema mjadala huo umekwishawekwa pembeni na kwamba Waziri Mkuu anakwenda kulishughulikia suala hilo kiutawala.
 
Juzi Bunge lilikataa kupitisha bajeti hiyo kutokana na msimamo wa wabunge wa pamoja kati ya wale wa CCM na wa upinzani hasa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukataa bajeti hiyo kwa maelezo kuwa haikuonesha suluhisho la tatizo la umeme nchini.
 
Kutokana na wabunge wengi kuikataa bajeti hiyo, Waziri Mkuu,Bw. Mizengo Pinda aliliambia bunge kuwa serikali itaondoa bajeti hiyo na kuifanyia marekebisho  na kuiwasilisha upya wiki tatu zijazo.

 



  

8 comments:

  1. naomba zitto kabwe na kamati yake warudi nyuma na kufanya scrutization ya pesa zooote zilizokuwa zinaflow kuja dodoma miaka yote katika wizara zooote ili kujua jinzi serekali inavyomisbehave na kubadilisha mwenendo mzima wa utendaji wa serekali

    ReplyDelete
  2. Nimesoma kwa kina article katika gazeti la Raia Mwema na kwa kweli ilikuwa ni taarifa ya Idriss Rashid kwa vyombo vya habari kuhusu Tanesco kununua mitambo ya Dowans. Kwenye paragraph ya pili kutoka mwisho ameandika nanukuu " Ni imani yetu kwamba tumeshajieleza na kujenga hoja za kutosha, na wananchi wa Tanzania watafanya maamuzi yao hapo ambapo nchi itakapokuwa imegubikwa na kiza, mahspitali hayatoi huduma, viwanda havizalishi, wanafunzi vyuoni wanashindwa kusoma kwa sababu tulishindwa kufanya maamuzi".

    Siasa za CCM za uraisi wa 2015 ndizo zinalitesa taifa kwa sasa. Serikali inaogopa kufanya maamuzi na kusikiliza porojo za wale jamaa wa CCJ (Sitta na Mwakyembe), sasa tupo hapa tulipo ambapo Dr Idriss alitabiri. Sasa nani wa kuchukuliwa hatua. Wananchi ni lazima tuamue sasa or never.

    Serikali ya CCM imechoka na imechoshwa na malumbano ya kisiasa ndani yao wenyewe, ndiyo maana huoni ajabu Mh Sitta kwenda Mbeya kwenye mkutano wa hadhara na kumsema vibaya waziri mwenzake (Ngeleja ) kana kwamba yeye si sehemu ya serikali. Ufalme wa CCM umefitinika na sharti uondolewe madarakani. Na hii si ya kusubiri 2015, tutakuwa tumechelewa mno, wanatakiwa waondolewe sasa tena kwa nguvu.

    Mungu ibariki Tanzania.

    ReplyDelete
  3. Hivi staili hii ya kila sekta ya kila wizara kuchangia imeanza leo au ndio za mwizi ni arobaini?Na ni wizara hii tu au ni zote zenye mtindo huu? Hakika maswali ni mengi,Je na ninyi wawakilishi wetu hapo mjengoni mwaka huu mgao ulikuwa mdogo mkaona muwalipue? Kwa nini ni nasema hivi sisi wananchi hatujui tangulini mlikua mnachukua bakishishi na kuzipitisha bajeti kwa vishindo na vigelele?
    Hivi hili sini sawa nalile la kampuni ya umeme tulilo ambiwa tunalidai pesa lukuki, lakini hatamae ikaonekana sisi ndio tunadiwa? Sintoshangaa kusikia kua waziri kasingiziwa na aombwe radhi, haya ndio maisha yetu ya COMMEDIAN.MUNGU TWAOMBA BARAKA ZAKO.

    ReplyDelete
  4. tatizo letu wa TZ TUNABLA BLAAAA!!!!!SONGI SONGI!!!!!!NYINGIIIIII!HIVI HILI LINA USHAHIDI SASA HAYA MAAMUZI MPAKA AKILI IPIGWE HENDELI INATOKA WAPI HII NI KWANZA ASIMAMISHWE KAZI NA UCHUNGUZI UFANYWE AKIWA NJE YA WIZARA.
    TUACHE TABIA YA KULINDANA HII NI RUSHWA YA HADHARANI KABISA HATA KIPOFU ANAONA.
    NCHI KAMA UINGEREZA ANGEJIUZLU NA TAYARI NAFUNGULIWA MASHITAKA IKADHIBITISHWE MAHAKAMANI.

    ReplyDelete
  5. uakaguzi wa kina ufanywe na CAG hili wataobainika wapelekwe mahakamani mara moja tumechoka na wizi wa kijima.

    ReplyDelete
  6. TAASISI ZOTE ZILIZOCHINI YA WIZARA ZIFANYIWE UCHUNGUZI WA DHARURA HASA KIPINDI HIKI CHA BUNGE.HUU NI UTAMADUNI WA ULAJI NA NI WA MIAKA NENDA RUDI SEMA WALIOKAMATWA NDIO HIVYO TENA ZA MWIZI AROBAINI .SASA KWA VILE WAMETUTOA USINGIZINI HII TABIA IKOMESHWE NA KUNA MBINU TU NYINGI ZA KUHAMISHA PESA KIPINDI KAMA HIKI UKAGUZI UFANYIKE KWA MAKINI SANA HII TABIA IKOMESHWE.

    ReplyDelete
  7. NITAMSAIDI CAG MAENEO YA KUKAGUA AFUATILIE NIGHT ALLOWANCE ZINZZOLIPWA KIPINDI HIKI MARA NYINGI NI MBINU CHAFU UTUMIKA KUKUSANYA PESA,UNUNUZI VIFAA HEWA KUTUMIA WAZABUNI,MATENGENEZO YA MAGARI HEWA KUTUMIA WAZABUNI HAPA ATAWAKAMATA VIZURI NDIO UFISADI ULIPO KATIKA MAENEO HAYA WIZARA MBALI MBALI SASA TUMECHOKA NA HAYA MAMBO WAKATI WANANCHI WANA PATA TABU WACHACHE WANATENGENA VITAMBI NA KUJILIMBIKIZIA MALI.

    ReplyDelete
  8. Naomba mforward kwa mwannchi nimeshindwa kutuma:
    :Ajali ya hood, mikumi

    Mawazo ya mkuu wa mbuga kuwa wanachoma moto ni kitu cha kawaida ni mawazo finyu, 'the end does not justify the means' si kwa vile haijatokea ajali basi mtindo wa kuchoma ni bora. Si sahihi hata kidogo! Kwanza uchomaji huua viumbe vengi kama fauna.
    Lazima hifadhi ishitakiwe na kuwafukuza viongozi wa hifadhi hiyo. Mikumi ni hifadhi isiyojitangaza ingawa ina wanyama wengi na kuweza kufikiwa kirahisi na wakazi wengi wa Dar-es-salaam. Fukuzeni hao!

    ReplyDelete