14 July 2011

African Lyon kusajili 'Maproo' wanne

Na Addolph Bruno

WAKATI usajili wa wachezaji ukitarajiwa kumalizika kesho, klabu ya soka ya African Lyon imesema inatarajia kukamilisha taratibu hizo kwa kuwasajili wachezaji
wanne wa kigeni.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Ofisa Habari wa klabu hiyo, Sherary Abdallah alisema wachezaji watakaowasajili tayari wapo nchini na mazungumzo yanafanyika baina yao na klabu hiyo.

Alisema ikiwa watafanikiwa kuwasajili wachezaji hao, watakuwa wamefanikisha kuziba nafasi zilizoachwa na wachezaji Idrisa Rashid aliyejiunga na Simba na Isaac Rajab, aliyekwenda Yanga hivi karibuni wakitokea katika klabu hiyo.

"Mpaka sasa tumewaacha wachezaji wawili ambao wameanza kambi na timu zilizowasajili, ambao ni Idrisa na Isaac kwa ujumla bado tunaendelea na usajili na tumefikia hatua nzuri," alisema Sherary.

Katika hatua nyingine, msemaji huyo alisema uongozi wa klabu hiyo bado unaendelea kuangalia uwezekano kwa timu yao kwenda kuanza kambi katika kitua chao cha nyumbani, ambacho bado hawajapeleka maombi kwa Shirikisho Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kuomba uwanja watakaoutumia kwenye wa Ligi Kuu.

No comments:

Post a Comment