17 October 2011

Magamba yazidi kuiandama CCM

*Nape asema bila kuyavua haraka nchi haitatawalika
*Asema wanaopinga wanafaidika na rasilimali za nchi
*Aonya wapambanaji wasipokuwa makini wanatolewa roho


Na Mwandishi Wetu, Mwanza

FALSAFA ya kuvuana magamba ncani ya Chama Cha mapinduzi (CCM) imezidi kukitesa
chama hicho na kuzua mvutano baina ya viongozi na baadhi ya wanachama sasa ikielezwa kuwa lazima mageuzi hayo yaendelee vinginevyo hali itakuwa mbaya na nchi itashindwa kutawalika.

Wakati kumekuwapo na msuguano na maelezo kuwa Katibu wa Halmashauri Kuu, Itikadi na Uenezi, Bw. Nape Nnauye anapotosha maagizo ya chama chake kuhusu dhana hiyo, yeye ameibuka na kusema mageuzi yanayoendelea ndani ya chama hicho maarufu kama kujivua gamba ni ya kweli, na yakifanyika ipasavyo ni ukombozi kwa wananchi wanyonge wa Tanzania lakini machungu kwa kundi linalofaidika na jasho lao.

Akihutubia mamia ya wananchi katika mkutano wa hadhara jijini Mwanza jana kwenye viwanja vya Magomeni, Kirumba, Bw. Nnauye alisema mageuzi hayo ni ukombozi kwa wanyonge kwa kuwa yamelenga kuimarisha misingi ya uadilifu na kuwajibika kwa viongozi waliopewa dhamana.

"Ni rahisi leo kumkuta kiongozi anamiliki utajiri wa kutisha na kufuru kuliko hata kipato chake halali, tukisema tukae kimya nchi hii haitatawalika. Dawa ni kufanya mageuzi haya leo kabla hali haijachafuka sana," alisema na kuongeza.

Kwa mujibu wa Bw. Nnauye, kufanikiwa kwa mageuzi hayo kutasaidia kuhakikisha kunakuwapo mgawanyo mzuri wa rasilimali za nchi, hivyo kulewa ukombozi wa moja kwa moja kwa wanyonge nchini.

"Tusisahau ndugu zangu, nguvu ya chama hiki na heshima yake imekuwa ni kutetea wanyonge nchini, Afrika na duniani kwa ujumla. Kutetea wanyonge lazima uhakikishe rasilimali za nchi zinanufaisha wanyonge, bila uadilifu na kuwajibika haitawezekana, ndio malengo ya mageuzi tuyafanyayo," alisema Bw. Nnauye.

Alisisitiza kuwa misingi ya CCM na imani yake vikifuatwa na kusimamiwa vizuri kwa dhati bila unafiki kelele zinazosikika leo za matumizi mabaya ya rasilimali za nchi hazitakuwepo na kuweka wazi kuwa kundi linalofaidika na hali ya sasa, ndilo linalopotosha maana ya mageuzi hayo kwa kutoa hoja alizoita dhaifu.

Alisema kumejengeka utamaduni na hasa kwa baadhi ya watu wenye dhamana kujijali wao wenyewe zaidi kuliko wananchi wanaowaongoza, tabia ambayo imeongeza tofauti ya kipato kati ya wananchi wa chini na viongozi wao, huku wengine wakiwa na kipato kisichokuwa na maelezo sahihi.

"Mwalimu (Nyerere) aliwahi kuwahoji viongozi waliotaka uongozi wa juu wakati huo, kwa umri wenu na kipato chenu mmetoa wapi utajiri huu? Na hiyo ilitosha kumzuia mtu asigombee uongozi, leo ukihoji uadilifu wa baadhi ya viongozi utaandamwa wewe, usipokuwa makini wanakutoa roho," alisisitiza Bw. Nnauye.

Akitoa ufafanuzi zaidi Bw. Nnauye alionya kuwa kama tofauti ya kipato isiposhughulikiwa mapema na hasa kuwadhibiti wale wanaojilimbikizia mali kwa njia haramu wakiwemo viongozi na kugeuza chama kichaka chao, nchi itavurugika kwa kuwa wanyonge ni wengi na watatumia nguvu kudhibiti rasilimali zao na kudai usawa.

7 comments:

  1. matendo hukidhi haja maridhawa kuliko maneno! Tunaweza kuongea mpaka machozi ya damu lakini km hatutendi huo unabaki unafi na unazidi kuwachosha na kuwakirihisha watu. Na zaidi sana maneno hayo matupu yanazidi kukuongezeeni maadui kuliko marafiki. Someni alama za nyakati. Inatosha kuona na kusikia ili uhukumu na wala haihitaji shahada ila common sense. Tekelezeni mnayoyasema.

    ReplyDelete
  2. nape na kikwete ni magamba pia

    ReplyDelete
  3. WATANZANIA MUELEWENI NAPE, ANA MAANA KUBWA ANAPO ZUNGUMZIA MAGAMBA.
    NA INAONEKANE HAO MAFISADI NDIYO TATIZO NDANI YA CHAMA HAPO BASI ISIWEPO UPENDO WA MTU KWA KIONGOZI FULANI AU KABILA! TUWE NA MAAMUZI WOTE KAMA WATANZANIA TUKIJUA KAMA KIONGOZI FULAN ATUFAI. NAUNGA MKONO KWA KUSEMA VIONGOZI MAFISADI WATOKE(WAVULIWE UONGOZI)AMBAO NDIO MAGAMBA. KAZANA NAPE WATANZANIA TUNAKUBARI KAZI YAKO.

    ReplyDelete
  4. Usidanganyike Nape, Tanzania sio CCM, magamba ni yenu CCM na viongozi wake. unapodai msipovuana magamba nchi haitatawalika unajidanganya! Tanzania bila CCM inawezekana. Kuwafukuza wakina Rostam na wenzake ndani ya Chama, haitawasaidia kitu. Kurudi nyuma hamuwezi wala kwenda mbele hamtafika popote. Mbona unawashupalia Mapacha watatu? Wakina Mkapa waliofanya biashara Ikulu wao siyo Magamba? Mwenyekiti wako hakutajwa katika orodha ya mafisadi 11 pale mwembe yanga mwaka 2007? yeye si Gamba linalostahili kuvuliwa? Samuel Sita ambaye yupo kwenye kundi lako, yeye si Gamba?

    Ninachofahamu mimi, yeye ndiye aliyesababisha suala la Dowans kufika hapa ilipo leo. Yeye ndiye aliyefunga mjadala wa Dowans usiendelee kujadiliwa Bungeni wakati wabunge wachache wa upinzani waking'ang'ania watuhumiwa wote wachukuliwe hatua. Sasa wewe unataka kumhadaa nani? CCM imekosa hoja ya kuwaambia watanzania zaidi ya kutapatapa kama mfa maji. Nape, nenda kajipange upya kwa hoja zako maana watanzania si wale wa mwaka 47, wanaelewa mbivu na mbichi. hata wewe mwenyewe hujiamini katika matamko unayoyatoa, ndio maana unazunguka nchi nzima kutafuta uungwaji mkono wa wananchi lakini wananchi hawapo katika vikao vya maamuzi ya CCM. Pole sana Nape kwa hili utavuna aibu! Tusubiri oune!

    ReplyDelete
  5. HUYU NAPE NDIYE MNAFIKI WA KWANZA GAMBA KUBWA NI KIKWETE ANAYEJILIMBIKIZIA MALI, ANAYEWAFANYA WATANZANIA WAPUMBAVU ANAJUA ANAMGAO WA PESA ZA DOWANS LKN ANATAKA SISI TUAMINI KWAMBA YEYE MTU SAFI! NAPE MBONA HUSEMI KIKWETE AONDOKE? AU UNAJIFANYA HUJUI UHUSIANO WAKE NA ROSTAM AZIZI NA NGELEJA NA KIKWETE? ACHA HIZO KUTUFANYA WAJINGA, KWANI NCHI ZILIZOINGIA VITANI UNAFIKIRI NIWAJINGA? NI MAMBO YA KIPUUZI KAMA YAKO KUJIFANYA MKWELI WAKATI MNAFIKI WA NGUVU

    ReplyDelete
  6. KIKWETE GAMBA KUBWA SANA, HUYU NA NAPE WANATAKIWA KUVULIWA NDANI YA CCM. NAPE WEWE UNA CHAMA CHAKE CCJ NENDA HUKO UNATAFUTA NINI CCM UNAUA WATANZANIA WETU! HAKUNA MAREFU YASIYOKUWA NA NCHI CCM IWE KWA KURA AU MTUTU WA BUNDUKI MTAONDOKA MABADILIKO HAYFANYWI NA WENGI BALI HULETWA NA WACHACHE NA KWA UMOJA WETU TUTAWAONDOA

    ReplyDelete
  7. NAPE NAPE, CHONDE CHONDE KAKA, WENGI TUMESHAKUSHTUKIA ETI msipovuana magamba nchi haitatawalika'' HIVI WEWE NI NANI HADI NCHI YA TANZANIA ISITAWALIKE? MI NAJUA UNAPENDA SANA KUTUMIA MANENO YA MW, NYERERE LAKINI NDANI HUIMANISHI HIVYO, WEWE NI MNAFIKI, ULIEVAA NGOZI YA KONDOO KUMBE NDANI MBWA MWITU, ULIKISALITI CCM UKAANZISHA CCJ, LEO UNAJIITA MKUBWA NA MSEMAJI WA CHAMA, NAPE WE NI MROPOKAJI SANA, MWENYE MAKUNDI NDANI YA CCM, UNATAKA KUWAGAWA VIJANA ILI UPATE FURSA YA KUWAPENYEZA WALA RUSHWA WENZANKO WAGOMBEE URAIS MWAKA 2015, NACHOTAKA KUKUAMBIA NI HIVI, MANENO YAKO YASIYO NA MASHIKO, DEBE HILO TUPU UNALOPIGA MWISHO WAKE NI 2015, HATA KAMA UTAKWENDA KWA KALUMANZILA, LAZIMA CCM IPIGWE CHINI. KILA SIKU UNAONGEA UPUPU UNATUMIA HELA ZA WALALAHOI KUZUNGUKA TANZANIA NZIMA KUWAELEZA WATU MAMBO YAKO YA KITOTO YASIYO NA MSINGI WOWOTE KATIKA JAMII. WATU WANAKUFA NJAA, UMEME WA MGAO, UCHUMI JUU, WANAFUNZI WANAKETI CHINI, BAA-DALA YA KUZUNGUMZA YANAYOTUHUSU, WEWE UNZUNGUMZIA UCHAGUZI.... NAKWAMBIA UTAANGUKIA PUA TU WE NGOJA

    ReplyDelete