02 October 2012

Uchaguzi CCM Ngwilizi chali, rushwa nje nje *Mgombea azirai, mtoto wa Wassira 'apeta' *Shitambala apita NEC, Mshangama aula



Na Waandishi Wetu

KINYANG'ANYILO cha kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kimeendelea kwenye maeneo mbalimbali nchini.

Upinzani mkali umejitokeza katika nafasi za Ujumbe wa Halmashauri Kuu (NEC), Mwenyekiti wa CCM na Mkutano Mkuu wa Taifa ambapo vigogo wengi wa chama wameangushwa.

Lushoto

Mbunge wa Mlalo, Wilaya ya Lushoto, mkoani Tanga, Brigedia Jenerali (mstaafu) Bw. Hassan Ngwilizi, ameangushwa vibaya na mfanyabiashara wa madini na mabasi, Dkt. Najim Msenga katika nafasi ya ujumbe wa NEC.

Dkt. Msenga alipata kura 895 wakati Bw. Ngwilizi alipata 651. Nafasi ya mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa, Bw. Majid Mwanga, aliibuka kidedea.

Nafasi ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya, Balozi Abdi Mshangama aliibuka kidedea baada ya kumshinda Bw. Matei Mbaruku wakati Bw. Shaaban Omar, akishinda nafasi ya Katibu wa Uchumi na Fedha Wilaya.

Bw. Mbaruku alipata kura 733, wakati Bw. Omar alipata 150, dhidi mpinzani wake Bi. Imelda Mchome aliyepata kura 29.

Mbunge wa Kilindi Bi. Beatrice Shelukindo, ameshinda ujumbe wa NEC baada ya kupata kura 812 kati ya 1,251 zilizopigwa. Bw. Kingalangala ameshinda nafasi ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya ambapo Bw. Suleiman Liwowa, mjumbe Mkutano Mkuu Taifa.

Sengerema

Mbunge wa jimbo hilo, Bw. William Ngeleja, ameshinda ujumbe wa NEC baada ya kupata kura 1,060 kati ya 1520 zilizopigwa akiwabwaga wagombea wenzake watatu.

Wagombea hao ni Dkt. Philemon Sengati ambaye ni Mhadhiri Chuo Kikuu cha Dodoma (132), Bw. Jowa Kasika (317) na Bw. Renatus   Nchali, mwalimu wa Shule ya Sekondari Sengerema (11).

Msimamizi wa uchaguzi huo, Bi. Helen Bogohe, alimtangaza Bw. Chasama Kamata kuwa Mwenyekiti wa CCM wilayani humo baada ya kupata kura 891 kati ya 1,520 zilizopigwa na kumshinda Bw. Jaji Tasinga, aliyekuwa akitetea kiti chake ambaye alipata kura 665.

Musoma

Msimamizi wa uchuguzi Wilaya ya Mosoma Mjini, mkoani Mara, Bw. Amos Sagala, alimtanagaza Bw. Daud Missango kuwa mshindi wa nafasi ya Mwenyekiti wa CCM Wilaya baada ya uchaguzi huo kurudiwa mara mbili na kupata kura 225.

Bw. Missango alimshinda Bw. Isack Chacha aliyapata kura 133, ambaye alizira baada ya kuomba kura zirudiwe siku ya pili.

Nafasi ya ujumbe wa NEC wilayani humo ilichukuliwa na Bw. Vedastus Mathayo aliyepata kura 346.

Baada ya kutangazwa mshindi, Bw. Mathayo, alitoa ahadi ya kuzifanyia ukarabati ofisi zote za kata.

Butiama

Msimamizi wa uchaguzi wilayani humo, Bw. Jackson Mang’ula alimtangaza Bw. Yohana Mnema kuwa Mwenyekiti wa CCM baada ya kumshinda Mwenyekiti wa zamani Nyabukika Nyabukika.

Bw. Christopher Siagi, alishinda ujumbe wa NEC wilayani humo ambapo wajumbe wa Mkutano Mkuu Mkoa ni Bw. Nestory Matiko na Rudia Mazera.

Morogoro

Mbunge wa Morogoro Mjini, Bw. Aziz Abood alichaguliwa kuwa mjumbe wa NEC ambapo baada ya uchaguzi huo, alisema chaguzi za ndani ya CCM zisitumike kuleta mpasuko badala yake viongozi wajiimarishe kukiwezesha chama hicho kuibuka na ushindi 2015.

Aliwataka wana CCM wote kuwa kitu kimoja kuhakikisha Mkoa huo unaendelea kuwa ngome ya chama hicho.

Bw. Sadiq Suleiman Murad, alichaguliwa kuwa mjumbe wa NEC Wilaya ya Mvomero ambapo Bw. Nasor Udelele alichaguliwa kuwa  Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kilosa. Bw. Omar Mgumba alichaguliwa kuwa mjumbe NEC Wilaya  ya Morogoro Vijijini.

Ilala kwafukuta

Katika hali inayoonesha matumizi makubwa ya fedha katika chaguzi za CCM bado tatizo, baadhi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu Wilaya ya Ilala, Dar es Salaam, walidai hali hiyo ndio iliyotawala kwenye uchaguzi uliomalizika juzi usiku.

Katika uchaguzi huo, diwani wa Kata ya Vingunguti, Bw. Assaa Simba, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti Mpya wa CCM wilayani humo baada ya kumbwaga vibaya Mwenyekiti anayemaliza muda wake Bw. Selemani Karanje.

Katika nafasi ya ujumbe wa NEC, mfanyabiashara mashuhuri jijini Dar es Salaam, Bw. Ramesh Patel, aliibuka mshindi dhidi ya wagombea wenzake watatu.

Wagombea hao ni Naibu Waziri wa Kazi na Ajira na Mbunge wa Segerea, Dkt. Makongoro Mahanga, ambaye ni mjumbe wa NEC anayemaliza muda wake.

Wakizungumza na gazeti hili jana, baadhi ya wapiga kura wa mkutano huo ambao hawakutaka majina yao yatajwe gazetini, walisema matumizi ya fedha yalikuwa makubwa hasa katika
nafasi ya ujumbe wa NEC.

Walidai madiwani karibu wote wilayani humo waliungana kumpinga na kumkashifu mgombea mmoja ambaye ni kiongozi wa kitaifa ambaye anafanya kazi na madiwani hao katika manispaa hiyo.

Waliongeza kuwa, baadhi ya madiwani waliitwa katika hoteli moja jijini Dar es Salaam (jina tunalo) wiki moja iliyopita na kuweka mikakati ya kummaliza kiongozi mwenzao.

“Kila diwani alipata kiasi kikubwa cha fedha na siku mbili kabla ya uchaguzi, mgombea husika aliwapeleka madiwani hao kwenye hoteli moja iliyoko Kigamboni nje kidogo ya jiji (jina tunalo).

“Wakiwa huko, walipewa fedha nyingine na kuweka mkakati wa kila diwani kuhakikisha wajumbe wa Mkutano Mkuu waliopo katika maeneo yao wanampigia kura mgombea husika,” kilisema chanzo chetu cha habari.

Walidai kuwa, madiwani hao walifanikiwa katika mkakati huo ambapo kabla ya uchaguzi, hali ilionesha wazi kuwa mgombea aliyewekewa mikakati ya kupingwa alikuwa na nafasi ya kushinda.

Hali ilibadilika usiku wa kuamkia siku ya uchaguzi ambapo baadhi ya madiwani na mbunge mmoja ndani ya Wilaya hiyo, walionekana kupita kwa wajumbe kabla kikao hakijaanza ili kuhakikisha mtu wao anashinda.

Wajumbe hao waliliambia gazeti hili kuwa, wakati wa mahojiano ukumbini, mjumbe mmoja alimwuliza Bw. Patel kuwa atawezaje kuwa mjumbe wa NEC Wilaya wakati hajui ofisi za kata na matawi ya chama kwenye kata mbalimbali.

Walidai pamoja na Bw. Patel kubabaika wakati akijibu maswali ya wajumbe, bado ameibuka na ushindi.

Baada ya matokeo kutangazwa, baadhi ya wajumbe walisikika wakisema “chama chetu kinakwenda pabaya kama wajumbe hawaangalii uwezo wa mtu kisiasa,”.

Kinondoni

KATIBU wa CCM wilayani humo, Bw. Edwin Milinga, alisema rushwa kwa viongozi wa vyama vya siasa ni changamoto kubwa inayokikabili chama hicho.

Bw. Milinga aliyasema hayo kwa njia ya simu wakati akizungumza na gazeti hili baada ya uchaguzi kumalizika ambapo Bw. Salum Madenge, aliibuka mshindi katika nafasi ya Mwenyekiti wa CCM na Bw. Kalisti Lyimo alishinda ujumbe wa NEC.

“Rushwa ni tatizo ambalo tumekuwa tukilishuhudia katika chaguzi kwa sababu baadhi ya wagombea hawajiamini, kila mmoja anahisi atendewi haki,” alisema.

Temeke

Mwenyekiti wa CCM wilayani humo alichaguliwa Sikunjema Shaban, ambapo mjumbe wa NEC ni Bw. Magesa Phares na Katibu wa Siasa na Uenezi Wilaya Bw. Chisumo Masuru.

Akizungumza na waandishi, Katibu wa CCM wilayani humo, Bw. Robert Kerenge, alisema mshindi wa nafasi ya Katibu Uchumi na Fedha Wilaya ni Bi. Hazal Issa.

Singida

Bw. Hamisi Nguli amechaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM akitetea nafasi yake katika kipindi cha miaka mitano mfulilizo baada ya kupata kura ya 287 kati ya 462 zilizopigwa na kumshinda Bw. Hassan Dumwala aliyepata kura 168 na saba ziliharibika.

Akitangaza matokeo hayo, Mjumbe wa NEC mkoani humo, Bw. Mohamed Misanga, alisema uchaguzi huo ulirudiwa baada ya wagombea wote kutofikisha nusu ya kura zilizopigwa.

“Awali Bw. Nguli alipata kura 287 kati ya 603, akifuatiwa na Bw. Dumwala (123), Bw. Mohamed Selemani (119) na Bw. Nkinde Omary alipata kura 76,” alisema na kuongeza kuwa, Bw. Hassan Mazalla alichaguliwa kuwa mjumbe wa NEC Wilaya ya Singida.

Bunda

Bw. Kambarage Wassira ambaye ni mtoto wa Mbunge wa Jimbo la Bunda Bw. Stephen Wassira, ameibuka mshindi katika nafasi ya ujumbe wa Mkutano Mkuu Taifa.

Nafasi ya Mwenyekiti wa CCM wilayani humo ilichukuliwa na Bw.  Chacha Kimanwa baada ya kumbwaga Mwenyekiti aliyemaliza muda wake Bw. Erasto Majura na Bw. Mramba Simba.

Msimamizi wa uchaguzi huo Bw. Maximilian Ngesi ambaye ni katibu Mwenezi CCM mkoani Mara, alimtangaza Bw. Bonfas Mwita kuwa mshindi wa ujumbe wa NEC.

Bw. Mwita aliwashinda Bw. Cyprian Msiba ambaye ni Mtangazaji wa Kituo cha Channel Ten na Bw. Daudi Iramba.

Chunya

Mbunge wa Songwe ambaye pia ni Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Bw. Philip Mulugo, alichaguliwa kuwa mjumbe wa NEC kupitia Wilaya ya Chunya.

Bw.Mulugo alijipatia zaidi ya 1,035, sawa na asilimia 82 ya kura zote zilizopigwa akiwashinda wapinzani wake Bw. Hamadi Juma Lema (66) na Polycap Ntapanya (364).

Aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM wilayani humo, Chakupewa Makelele, alifanikiwa kutetea kiti chake baada ya kupata kura 785 dhidi ya 716 alizopata mpinzani wak, Bw. Noel Chimwaga.

Akizungumza baada ya uchaguzi kumalizika, Bw. Mulugo alisema atatumia nafasi hiyo kuwatumikia wananchi wote wa Chunya tofauti na ilivyokuwa awali sambamba na kusambatarisha upinzani hasa katika Jimbo la Lupa.

Kwa upande wake, Bw. Makelele aliwashukuru wana CCM kwa kuendelea kumwamini na kumchagua hivyo atapeperusha bendera ya chama hicho ili kiibuke na ushindi mnono 2015.

Katika uchaguzi huo, Mtunza Hazina wa Halmashauri ya Wilaya hiyo, Bw. Frank Chonya, aling’ara baada ya kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa na mjumbe wa Mkutano Mkuu Mkoa kutoka wilayani humo.

Mbozi

Bw. Aloyce Mdalavuma, alichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM Wilaya baada ya kupata kura 602, akifuatiwa na Bw. Laurent Mgalla (298), Bw. Maliki Nzowa (119) na Bw. Bryceson Simwinga (27).

Nafasi ya mjumbe wa NEC wilayani humo ilichukuliwa na Bw. George Mwenisongole aliyepata kura 830 dhidi ya wapinzani wake Bw. Israel Msonganzila (88) na Bw. Yusuf Mgogo (66).

Mbeya Mjini

Wakili maarufu Bw. Sambwee Shitambala, alipata ushindi mkubwa wa nafasi ya ujumbe NEC ambapo Bw. Ephraimu Mwaitenda akichaguliwa kuwa Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Mbeya.

Mbeya Vijijini

Aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM wilayani humo Bw. William Simwali, ameangushwa na Bw. Ipyana Seme ambaye awali alikuwa Katibu wa CHADEMA wilayani humo.

Habari hii imeandikwa na Yusuph Mussa, Faida Muyomba, Veronica Modest, Ramadhan Libenanga, Anneth Kagenda, Kassim Mahege, Raphael Okello,  Damiano Mkumbo, Esther Macha, Rashid Mkwinda.

2 comments:

  1. Rushwa ndani ya chama tawala inatishia usalama wa walio wengi nje ya chama kwani hao wala rushwa wakiingia madarakani wanatuongoza sote bila kujali mwanachama wa CCM na asiye mwanachama. Anyway, sina cha kushangaa sana kwani kama wakuu wa ngazi za juu wanatoa na kupokea rushwa, ni wazi hata wa chini watafanya hivyo. Nyere akifufuka leo atatamani tufe sote kije kizazi kingine sikivu kwani alishahubiri sana haya lakini hatusikii. MUNGU MBARIKI KIKWETE, MUNGU YABARIKI MAFISADI. AAAAAMEN

    ReplyDelete
  2. CCM NI CHAMA MAKINI MAANA INADHIHIRISHA BAADA YA CHAGUZI ZAKE KUSIKIKA KILA KONA YA NCHI NA NINGETOA USHAURI KWA VYAMA VINGINE VYA SIASA KAMA CHADEMA NA NCCR MAGEUZI, NA NINGESHAURI WAWE WANAFANYA UCHAGUZI NAO TUMEWAZOEA KILA MARA AKINA LIPUMBA NDO WANAGOMBEA HATA UKIFANYIKA UCHAGUZI HAUWI HURU KAMA INAVYOTAKIWA , NARUDIA MANENO YA MWALIMU ALISEMA HAKUNA CCM BORA KAMA HAKUNA CHAMA PINZANI BORA, BY kevin isaya

    ReplyDelete