15 July 2011

Wizara yaimarisha mafunzo kuongeza walimu wa sayansi

Na Mwajuma Juma, Zanzibar

WIZARA ya Elimu na Mafunzo ya Amali, imesema imeimarisha mafunzo ya Stashahada na Shahada ya walimu wa masomo ya sayansi ili kuongeza idadi ya walimu wenye
sifa za kufundisha somo hilo katika shule mbalimbali.

Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Bi. Zhra Ali Hamad, aliyasema hayo jana wakati akijibu swali la Mwakilishi wa Jimbo la Tumbe Bw. Rufai Said Rufai, katika Kikao cha Bajeti cha Baraza la Wawakilishi kinachoendelea mjini Zanzibar.

Alisema mpango huo utainua kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wanaosoma mafunzo hayo kutokana na uhaba mkubwa wa walimu wenye sifa na kuongeza kuwa, Wizara inaandaa mafunzo kazini kwa walimu wa sayansi kupitia vituo vya walimu.

“Mafunzo haya yatakuwa ya miezi sita, Wizara inakusudia kutoa mafunzo kwa walimu 500 wa sayansi na tayari zaidi ya walimu 300 wamepatiwa mafunzo ya awali,” alisema.

Katika swali lake, Bw. Rufai alitaka kujua Wizara hiyo imeandaa utaratibu gani ili kuondoa tatizo la kufeli kwa wanafunzi wa sayansi, hali ambayo imechangiwa na ukosefu wa walimu wenye sifa.

No comments:

Post a Comment