18 July 2011

Serikali iunde chombo kutatua kero sekta ya elimu' Moshi, KILIMANJARO

Na Gift Mongi

WITO umetolewa kwa Serikali kuunda chombo ambacho kitatatua kero mbalimbali zilizopo katika sekta ya elimu hasa katika shule za msingi na sekondari ili Taifa lipate wasomi
wazuri kuliko ilivyo sasa.

Akizungumza mwishoni mwa wiki mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro katika maadhimisho ya miaka 10 ya mfuko usio wa kiserikali wa New Life Foundation (NLF), Askaofu wa Kanisa la TAG, Jimbo la Kilimanjaro, Glorious Shoo, alisema sekta hiyo inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinahitaji kupatiwa ufumbuzi ili kuinua kiwango cha elimu nchini.

Askofu Shoo ambaye pia ni rais wa mfuko huo, alisema wapo baadhi ya watumishi katika sekta hiyo ambao sio waaminifu ambao wamekuwa wakitoa mitihani kwa wanafunzi kabla haijafanyika jambo linalokwamisha maendeleo ya elimu nchini.

“Huwezi kusema mtoto amefaulu na kuchaguliwa kujiunga kidato cha kwanza alafu hajui kusoma wala kuandika sasa aliwezaje kufaulu mtihani,” alisema Askofu Shoo.

Aliongeza kuwa, usahihishaji mitihani hasa ya kitaifa si mzuri kutokana na udanganyifu uliopo wa kupendelea baadhi ya wanafunzi kwa kupwa alama kubwa ili waonekane wamefaulu jambo linalokatisha tamaa wanafunzi wenye uwezo kielimu.

“Jambo la msingi ni kuwepo kitengo maalumu ambacho kitaiwezesha Serikali kutatua changamoto zilizopo kwa wakati baada ya kuwafikia walengwa,” alisema.

Katika hatua nyingine. Askofu Shoo alitoa wito kwa Serikali kuwa makini na tatizo hilo na kulifikiria kwa mapana kwani nguvu ya sekta hiyo haipo katika ukaguzi wa majengo pekee bali ni pamoja na kuzifanyia kazi changamoto hizo.

No comments:

Post a Comment