08 April 2011

UDOM watawanywa kwa mabomu bungeni

Na Edmund Mihale, Dodoma

ASKARI wa Kikosi cha Kuzia Fujo (FFU) jana, walilazimika kutumia mabomu ya machozi na risasi kuwatawanya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma na
wanaharakati wengine baada ya kufunga barabara kuu ya kutoka Morogoro ili kulishinikiza waruhusiwe kuingia kwenye eneo la kushiriki mjadala Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba.

Wakizungumza katika lango kuu la  Ofisi za Bunge majini Dodoma  jana kwa nyakati tofauti wanafunzi hao walisema kuwa ni jambo la kushangaza kwa ofisi hiyo kuwaalika wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya City na kukiacha chuo hicho bila ya kuwa na uwakilishi.

"Muswada huo umeandikwa kwa lugha ya Kiingereza wamealika wanafunzi wa Shule ya Sekondari City ambao hawajui Kiingereza shule yenye matokeo mabovu kila mwaka, huku ni kuwachezea wananchi, alisema mmoja wa wanafunzi hao.

Mmoja ya wanafunzi hao ambaye alijitambulisha kwa jina la moja la Denis, alisema iwapo wabunge watapitisha muswada huo wako radhi kuingia mtaani kupinga tume hiyo kwa kuwa haiwezekani kufanya majadiliano katika mikoa mitatu ya Zanzibar, Dar es Salaam na Dodoma, ilihali kuna mikoa mingi inatakiwa kuwasilisha maoni yake.

"Hawa wabunge wakipitisha mambo hayo tutashtaki kwa wananchi na kisha tunahamia mtaani tunafanya kama ilivyo Tunisia, Libya na Misri lazima kieleweke," alisema mmoja wa wanafunzi hao kwa kipaza sauti.Alisema kuwa muswada uliowasilishwa bungeni na serikali chini ya hati ya dharura haukidhi mahitaji ya Watanzania.

"Watanzania wa leo sio wa juzi au jana, hatutaki kijitabu chenye maandishi kinachoitwa katiba bali makubaliano ya utaratibu wa jinsi ya kuendesha maisha yetu katika nchi hii kwa kujadiliana kila kitu jambo linalohusu kwa manufaa ya wote, kwa haki na usawa ulioandikwa katika kitabu kitakachokuwa na kumbukumbu ya makubaliano. 

"Kwa matiki hii rasmu ya serikali inaonesha kuzidisha matatizo badala ya kuyapunguza kwa kuwa inaonesha kuwepo kwa kikundi cha watu wachache wanaotugilibu na kujitengenezea katiba ya kujilinda wao na mambo yao kwa manufaa yao. Tena wanaonesha kuwa wananufaika kwa sisi kupata shida, kwa kuwa ukisoma utagundua katika yale matatizo yetu makubwa hawataki tujadili kwa pamoja na kuyatatua," alisema.

Hata hivyo, hotuba hizo zilikatishwa baada ya kujitokeza kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dkt. James Msekela ambaye alijikuta katika wakati mgumu kwa kuzomewa na wanafunzi hao.

"Mtoe huyo mtoe huyo mtoe huyo alitupiga mabomu, hatumtaki anaongea pumba, pumba, pumbaaaa pumbaaaa," walisikika wanafunzi hao wakisema kwa jaziba.

Dkt. Msekela alishindwa kutuliza fujo hizo hadi alipojitokeza  Mbunge wa Arusha mjini, Bw. Godbless Lema ambaye alipokewa kwa shangwe na vigelegele, 'jembee, jembee, jembee zilisikika sauti za wanafunzi hao.

Baada ya kuwashusha munkari, Bw. Lema aliwataka wanafunzi hao kuacha jazba, lakini aliulaumu utaratibu uliowekwa na bunge kwa kuwa haukuwatendea haki wananchi wanaoishi katika Mkoa wa Dodoma na migine kwa kutumia ukumbi mdogo wakati wakijua kuwa wananchi wana shauku ya kutoa maoni yao kwenye muswada huo.

"Nimewaita wanafunzi wa chuo kikuu ili kuja kujadili muswada huu kwa kuwa umeandikwa kwa lugha ya Kiingereza, hivi muuza mchicha, bagia anaweza kujadili muswada huu? Kuna watu wangapi wanapenda kuja hapa kujadili mustakabali nchi yao, hamuwezi kuita watu 300 ambao ni sawa na idadi ya wabunge wote," alisema Bw. Bw. Lema.

Alisema kuwa bora ofisi hiyo ikatafuta sehemu nyingine kubwa itakayoshirikisha watu wengi kujadili muswaada huo na kutoa maoni yao kwa uhuru kuliko kufanya katika chumba kidogo na kuwanyima haki watu wengine.

Mazungumzo hayo yalikatishwa na vurugu za wanafunzi hao waliotaka majadiliano hao yafanyike katika Uwanja wa Jamhuri, jambo lilopingwa na Dkt. Msekela ambaye alitaka kufanyika katika ukumbi wa Chimwaga.

Wanafunzi hao walipiga kelele kushinikiza kufanyika katika uwanja huo huku wakirusha mawe na kumzomea ndipo, Dkt. Msekela alipoamru Jeshi la Polisi kuwatanya, jambo lilozua kizazaaa katika mitaa mbalimbali ya mji wa Dodoma. 

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya vurugu hizo, Dkt. Msekela alisema kuwa ameamua kufanya hivyo kutokana na kushindwa kuelewana na wanafunzi hao, huku akimrushia lawama, Bw. Lema kuwa ndiye chanzo cha vurugu hizo.

"Ninatoa onyo kwa wanasiasa wanaojihusisha na siasa katika Chuo Kikuu cha Dodoma nimeambiwa kuwa jana kuna mwanasiasa mmoja alikwenda kule kuwahamasisha wanafunzi hawa," alisema Dkt Msekela.
 
Baada ya kusikia hivyo, Bw. Lema, alisema kuwa hakuna haja kuuma maneno, bali yeye ndiye aliyekwenda katika chuo hicho na kuzungumza na wanachama chama chake na atarudi tena Jumamosi.

"Mie ndiyo nilikwenda huko na kuzungumza na wanachama wangu na Jumamosi nitakwenda tena, njoo tutakutana tusitishane, si muda wa kutishana. Nimekwenda nikafanya siasa nje ya maeneo ya chuo sasa tatizo langu nini," alisema Bw. Lema. Baada ya kauli hiyo, Dkt. Msekela alionekana kunywea.

9 comments:

  1. Ya.mimi sishangai kuona hali hii ya wasomi kuzuiwa kwani watanzania mmesahau ni serikali hii hii iliyowanyima wanachuo haki ya kupiga kura kwa kudai anayetaka apande gari aende alipojiandikishia...mi nadhani mfumo wa wanasiasa wa kiafrika kuhofia wasomi ndio huo unatufikisha hapo.Udom tuakilisheni nyie mlio karibu na mjengoni...Mungu wabariki wote wenye mawazo mema na TZ

    ReplyDelete
  2. by grace;
    kama uchangiaji wa mawzo ya katibani huru na wazi, kwa nini wanavyuo wanazuiwa? kila mmoja anatakiwa kuchangia bila kutumia uwakilishi uliobuniwa kwa makusudi ili kuharibu taswira halisi iliyokusudiwa.
    kwa mustakabali huo, wanaozuia wana vyuo wasiingie inaonesha walikuwa na watu maalum waliowaandaa ili kuwakilisha kilichoandaliwa, na kuna habari ambazo wapo wa2 maalum waliochomekwa ili kuwakilisha majumuisho yasiyo na lengo halisi.maandalio hayo ya kundi dogo,baada ya habari kuvuja na kugundulika, ndiyo yamesababisha wanavyuo kutotulia na wao kuhitaji nafasi. hivyo ndivyo ilivyo, tusidanganyane.

    ReplyDelete
  3. Kwa kweli nchi hii viongozi wa chama tawala wanataka kuleta vurugu.Kwani wanahofu nini uundwaji wa katiba mpya. Ninachofahamu ni kuwa katiba ya nchi ndiyo sheria mama ya kila kitu.Hawa watu wasitengeneze hati ya dharula kutaka kutufisha ambako siko wabunge wa chama tawala naomba mjadiliane kwa kuangalia maslahi ya wananchi waliowatuma kuwakilsha katika bunge mjue mkifanya haya mambo kwa ushabiki wa chama mkaye mkijua 2015 hata kwa katiba hiyo mbovu hamtapita labda mchakachue sana.kitu ambacho kitakuwa ni kigumu watu watalinda masanduku ya kura.Chondechonde wabunge wa chama tawala jadilini huu mswada kwa manaufaa ya watanzania na si vinginevyo.

    ReplyDelete
  4. Kwa vile kumbi zilizoandaliwa ni ndogo kulingana na jumla ya watu wanaotaka kushiriki na umuhimu wa kazi yenyewe, basi mijadala ifanyike katika maeneo mengi na wawakilishi wachaguliwe kati yao ili kuwakilisha maoni yao. Mchango wa wasomi, wafanyakazi, na idara nyingi ni muhimu, hivyo kuwepo na vituo mabali mbali vya kukusanya maoni na baadye yawekwe pamoja na tume huru. Huwezi kuweka mijadala ya namna hii katika sehemu wazi na kwenye watu wengi kwani muda utatuminka mwingi na mawazo yanapishana. Kwa mfano, Walimu wa vyou vikuu wangejipanga pamoja na wanafunzi wao wajadili mswada na wachague wawakilishi wa maoni katika tume huru. Sioni sababu ya watu kuvamia ukumbi. Wabunge tumieni busara kupanga namna ya kuongoza mijadala. Mbona ktk kujadili mishahara yenu hatusikii fujo?

    ReplyDelete
  5. wasomi gani uchwara chuo hakina hata hadhi za kimataifa?vitanda dabodeka utafikiri sekondari du mue na aibu tatizo vyuo vya kuongea vimezidi hapo bongo mbona muhimbili hao wanasiasa hawaendi?nani ataacha kusoma akamsikilize mwana siasa?hatuwasikii hata maprofesa wa kweli ambao wote wapo muhimbili kujihusisha na vyama?lkn hao maprofesa wa kozi za kuongea ndio wenyewe kila kitu wanajua wenyewe nchi hiyo umasikini utaisha kweli? ama kweli inasikitisha maana kwa sisi tulio ughaibuni tunaona maprofesa wanavyo fanya kazi zao za kitaaluma sio siasa wana tunga vitabu na ndio vinavyotumika mashuleni lkn sio kwetu vitabu hakuna mpaka tupewe msaada maprofesa tunao wanafanya kazi gani?

    ReplyDelete
  6. Viongozi wa ccm wote ni mbumbumbu. Yaani mnashindwa kusoma alama za nyakati.. nawasikitikiea sana. Mnatafuta mchawi wa vurugu za kujadili katiba na mnadhani kuwa mchawi ni chadema au mbunge G. lema. Huu uhuru na haki wa kila mtanzania kutoa maoni yake umetoka wapi? Mswaada wenyewe umeandikwa kwa kiingereza kwa makusudi ili kuwaondoa kwenye majadiliano asilimia kubwa ya Watanzania ambao mnajua hawajui klugha hiyo. majadiliana yanafanyika katika kumbi ambazo hazimudu idadi kubwa ya watu. Huu uhuru wa watanzania wengi kujadili mswada huu utafanyika vichakani au kwenye vilabu vya pombe ikiwa hakuna mazingira mazuri ya kuchangia mswada huu. Tunaomba usituletee kichefuchefu.
    gazeti lako siku zote linabezi kutetea CCM tu ambao sasa wanataka kuchakachua mswada wa katiba mpya. Na ndiyo maana akina Prince Bagenda, Tambwe Hizza .. na mzee warioba walizomewa hovyo! Someni alama za nyakati.. watanzania wamechoka na uchakachuaji wenu! Mnakwenda kwenye mijadala wa mswada wa hamsemila maana ila mnamjadili rais ambaye ameonyesha wazi nia ya kuchakachua kupatikana kwa katiba...bohhh! Msizomewe!!

    ReplyDelete
  7. wewe uliyechangia maoni muda 9.32 ndiye uchwara! nchi ambayo hata baada ya miaka 50 ya uhuru haina umeme na maji unataka iwe na vyuo vyenye vitanda vya vioo! Nchi itaendeleakuw maskini kam wasomi hawatajihusisha na siasa.Na si kweli vitabu havitungwi, tatizo hata vile vichache vianvyotungwa havipati sapoti ya serikali.DAWA YA MATATIZO YETU SI KUWAACHIA WATU MBUMBUMBU WAENDELEE KUTUONGOZA BALI NI KILA MMOJA (HASA WASOMI)N KUJIHUSISHA NA SIASA KWANI HATA DAKTARI, PROFESA WA MUHIMBILI UFANISI WAKE UNAATHIRIWA NA SERA ZA WANASIASA

    ReplyDelete
  8. Mswada huu utakuwa na maaana kama watu wote watachangia kwa naman ambalimbali. Vitolewe vipeperushi mbalimbali vya kudondoa vipengere kimojakimoja visambazwe, machapisho pia kwenye magazeti juu ya mswada huo yawekwe, watu wasome na watoe mawazo yao, vipindi vya redio na television virushwe kueleza mambo muhimu kwenye mswada ili kila mtanzania aelewe. Zaidi uwekwe kwa lugha ya taifa, mbona kampeni na mabango ya uchaguzi mkuu yaliandikwa kiswahili? hili la mswada liweje kiingereza ambapo wengi hawajui?

    ReplyDelete
  9. KUNA KUPITISHA MSWADA WA KUTUNGA KATIBA NA KUCHANGIA MJADALA NA KUTOA MAONI KUHUSU MFUMO WA KATIBA MPYA,HAPA KUNA KIKUNDI CHA WANASIASA WANAOJIPANDIKIZA KUJIFANYA KATIBA NI HAKI YAO PEKEYAO NA NDIO WANAWARUBUNI BAADHI YA WANACHUO KUSHIRIKI KTK KUANZISHA VURUGU,MAANA SASA IMEKUWA NI NJIA YA KUJIFANYA WAO WANASIKILIZWA SANA NA BAADHI YA HAO WASOMI,NA PIA NDIO AKISIMAMA MCHANGIAJI YYT WA CHAMA TAWALA AZOMEWE NK KWA MWENDO HUU HATUTAPATA UFUMBUZI MAANA KILA KITU WANADAI NGUVU YA UMMA MARA MAANDAMANO MPK KIELEWEKE HV SHIDA NA MATAKWA YAKO YAKULAZIMISHA FUJO NDIO UFUMBUZI?AU KUSEMA MPK KIELEWEKE IWE KAMA MISRI,TUNISIA AU SYRIA HIVI MPK SASA HUKO MNAKOTOLEA MIFANO KIMEELEWEKA AU NDIO WAMEKUWA WAKIMBIZI KTK NCHI ZAO? TUWE MAKINI MTANDAO HUO WA FUJO HAO VIONGOZI WANAOWARUBUNI WANALIPWA HELA NYINGI SANA NYINYI MNAAMBULIA MABOMU YA MACHOZI HAYA JITAHIDINI KWA MWENDO HUO MTAFIKA..!!

    ReplyDelete