19 August 2013

AZAM YAIPA SOMO YANGA

  • MECHI YA NGAO YA JAMII YAINGIZA MILIONI 208/-


Na Amina Athumani
UONGOZI wa Mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara Yanga umesema kwa sasa utajipanga upya baada ya mchezo wa juzi dhidi ya Azam.Mchezo huo wa Ngao ya Jamii ambao ni kiashiria cha msimu mpya wa ligi 2013-14, ulichezwa jana kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, ambapo Yanga ilifanikiwa kushinda bao 1-0.

Meneja wa timu hiyo Hafidhi Salehe alisema kwa sasa sio kipindi cha kulegalega kwao kwani wanahitaji kujiandaa vya kutosha katika dakika hizi za mwisho ili kuhakikisha wanafanya vizuri katika ligi hiyo.
Salehe alisema timu hiyo itaendelea na ratiba yao ya mazoezi leo katika uwanja wa shule ya Loyola, huku wakihakikisha wanafanya mazoezi ya hali ya juu ili kuhakikisha wanaingia katika msimu mpya wakiwa fiti zaidi.
"Ingawa tumeanza vizuri katika mechi hii ya kukaribisha ligi, lakini tunahitaji mazoezi zaidi kabla ya kujitupa uwanjani Agosti 24 kuanza ligi na kwa mujibu wa kocha mkuu Ernie Brants ni lazima timu ipate mazoezi ya ziada ili kuhakikisha tunatetea ubingwa wetu," alisema.
Aliongeza kuwa kwa upande wa wachezaji ambao waliinua katika mchezo huo Kelvin Yondani na Ally Mustapha wanatarajia kujiunga na timu kuanzia kesho kutokana na hali zao kuendelea vizuri lakini wachezaji wengine waliosalia wapo fiti.
Wakati huo huo, mechi hiyo ya Ngao ya Jamii iliyochezwa Agosti 17, mwaka huu Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 208,107,000. Washabiki 26,084 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo ambayo ilimalizika kwa Yanga kuifunga Azam bao 1-0.
Mgawanyo wa mapato ya mechi hiyo uliokuwa kama ifuatavyo, asilimia 18 ya kodi ya ongezeko la thamani (VAT) sh. 31,745,135.59, asilimia 10 ya mchango wa kusaidia jamii sh. 20,810,700, gharama ya tiketi sh. 7,309,866.
Uwanja sh. 22,236,194.76, gharama za mchezo sh. 13,341,716.86, Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 5,188,445.44, TFF sh. 13,341,716.86 na Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 6,670,858.43. Kila klabu imepata mgawo wa sh. 43,731,183.0
 


No comments:

Post a Comment