16 July 2013

WAFUGAJI PWANI WATAKIWA KUJIUNGA IPASO


 JAMII ya wafugaji mkoani Pwani wameshauriwa kujiunga na Mtandao wa Wafugaji Mkoa wa Pwani (IPASO) kwa lengo la kuongeza umoja utakaowawezesha kufanikisha mambo mbalimbali ya kimaendeleo ikiwemo sekta ya elimu, anaripoti Omary Mngindo, Bagamoyo.
Rai hiyo imetolewa na mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma, Bi.Keyana Kimunyu kwenye mkutano ulioandaliwa na umoja huo na kuhudhuriwa na wafugaji zaidi ya 100 uliokuwa chini ya mwenyekiti wake, Bw.Letoni Leboi.

Bi.Kimunyu alisema kuwa jamii ya wafugaji pamoja na kuwa na nafasi nzuri kiuchumi kutokana na wengi wao kumiliki mifugo, lakini cha kushangaza hawatambui umuhimu wa elimu hivyo kushindwa na jamii ya wakulima ambao wanategemea kilimo kusomeshea watoto wao.
Alieleza kuwa kwenye chuo kikuu anachosoma mkoani Dodoma, wanafunzi jamii ya wafugaji hawazidi 15 na kuwa katika mahafari yaliyopita ni mwanafunzi mmoja tu wa kifugaji aliyehitimu elimu chuoni hapo hali inayothibitisha kuwepo kwa upeo mdogo kwa jamii hiyo kwenye sekta hiyo ya elimu.
Mwanafunzi mwingine aliyethibitisha kauli ni Bi. Neema Mahungu ambaye alielezea masikitiko yake kutokana na yeye kufanya vizuri katika elimu yake kidato cha sita lakini mzazi wake ameshindwa kumwendeleza kielimu huku akimtaka mwanafunzi huyo aolewe.
“Cha kushangaza pamoja na kufanya vizuri katika masomo yangu katika shule ya Eaboishu iliyoko jijini Arusha, mzazi wangu amenieleza hana uwezo wa kuniendeleza zaidi kielimu huku akinitaka niolewe na tayari ameshanitafutia mchumba,” alisema mwanafunzi huyo.
Kwa upande wake Bw.Sheder Mkole alikuwa wa kwanza kutoa ushauri wa kuanza kuendeshwa kwa harambee kabla ya kuendelea na mkutano huo ulioitishwa na umoja huo wa wafugaji mkoani Pwani kwa lengo la kujadili mambo mbalimbali ya kimaendeleo.
Mratibu wa Umoja huo Bw. Lekope Laini amewaeleza wana-IPASO hao kwamba lengo kubwa la umoja huo ni kuhakikisha jamii ya wafugaji wanakabiliana na changamoto mbalimbali zinazowakabili.
Katika harambee hiyo zimekusanywa kiasi cha sh. 720,000 ambapo kati ya hizo sh. 130,000 ni taslimu huku ahadi zikiwa sh. 570,000.

No comments:

Post a Comment