22 July 2013

VIELELEZO VYA KESI VYAIBIWA POLISI



Na Daud Magesa, Mwanza
WATU wasiofahamika idadi yao wanaodhaniwa wezi,wameiba vielelezo katika stoo ndogo ya Kituo Kikuu cha Polisi Kati, Wilaya ya Nyamagana, mkoani Mwanza baada ya kuvunja madirisha.Tukio la wizi huo lilifanyika Julai 15, mwaka huu, majira ya usiku wa kuamkia Jumatano katika jengo la Polisi Wilaya ya Nyamagana.Akizungumza na gazeti hili jana, Kamanda wa Polisi Mkoa Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Ernest Mangu, alisema wezi hao kabla ya kuingia ndani ya jengo hilo ,walivunja dirisha la ofisi za Elimu, Ukaguzi Kanda ya Ziwa.

Alisema baada ya kufanikiwa kuingia ndani ya ofisi hizo, hakuna walichoiba ndipo walivunja dirisha na kuingia kwenye ofisi za Polisi Nyamagana.Alisema walivunja dirisha na kutanua nondo kwa jeki na kisha kuingia kwenye stoo hiyo ndogo ambamo vielelezo hivyo vilitunzwa.
Aliongeza kuwa baada ya kuingia ndani ya stoo hiyo waliiba begi moja la nguo na kompyuta mbili mpakato,moja ya kompyuta hizo ni kielelezo katika kesi ya ujambazi ambayo mtuhumiwa alikamatwa nayo, ambaye kwa sasa yuko mahabusu katika Gereza Kuu la Butimba.Kamanda Mangu alisema kompyuta ya pili ni kielelezo cha kesi ya uharibifu wa mali inayomkabili fundi mmoja na begi la nguo ambazo mwenyewe nazo hafahamiki.Alisema liliokotwa na polisi baada ya kuwakurupusha wezi ambao walikimbia na kulitelekeza.
Alieleza kuwa eneo walikopitia wezi hao usalama wake ni mdogo kwani ni uchochoroni na hakuna ulinzi wala mwanga wa taa, hivyo wanajaribu kuangalia nani mmiliki wake kama litakuwa ni mali ya taasis
i za serikali basi liendelezwe ili kuboresha usalama wa hapo na maeneo jirani.

No comments:

Post a Comment