17 July 2013

TUGHE YAKEMEA RUSHWA KWA WATUMISHI



 Na Livinus Feruzi, Bukoba
WAFANYAKAZI wa Serikali Kuu na Afya kote nchini, wametakiwa kuacha tabia ya kuomba na kupokea rushwa mahala pa kazi na badala yake watekeleze wajibu wao kwa kufuata kanuni, taratibu na sheria za kazi.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali Kuu na Afya Tanzania (TUGHE), taifa Bw. Ally Kiwenge wakati akizungumza na viongozi wa chama hicho na wafanyakazi wa idara ya afya, katika ziara yake ya siku moja aliyoifanya kwenye Wilaya za Muleba na Bukoba.

Bw.Kiwenge alisema kuwa w a n a c h a m a w a TUGHE wakiwamo watumishi wa hospitali, mahakamani, magerezani na polisi wanalalamikiwa kwa kula rushwa mahala pa kazi na kuwa tatizo hilo litasimamiwa na chama hicho ili kuondoa aibu iliyopo hivi sasa.
"TUGHE haiwezi kuwa kichaka cha kuficha walarushwa, wazembe kazini, makatibu wa mikoa simamieni hili kuanzia ngazi za matawi hakuna anayeweza kujificha kwa kula rushwa asitambuliwe," alisema katibu huyo wa TUGHE taifa.
Alisema kuwa, pamoja na kuwa wanawahimiza waajiri kuwalipa waajiriwa stahili zao, lakini pia lazima waajiriwa watimize wajibu wao kwa mujibu wa taratibu na kuwa TUGHE haipo kwa ajili ya kuchochea migogoro kazini, bali kuleta maelewano kwa pande zote.
Akizungumza na ujumbe wa TUGHE ofisini kwake, katibu tawala wa Mkoa wa Kagera, Bw. Nassor Mnambila alikiri kuwepo kwa malalamiko ya wananchi kuombwa rushwa na watumishi na kuwa serikali inajitahidi kukabiliana na kero hiyo.
Bw. Mnambila alisema kuwa mbali na hilo pia kuna baadhi ya viongozi wa vyama vya wafanyakazi ambao wanajifanya kama viongozi wa vyama vya siasa na kusababisha uchochezi wa migororo mahala pa kazi, ambapo aliwataka kubadilika.
Awali, akisoma taarifa ya TUGHE, katibu wa chama hicho Mkoa wa Kagera, Bw. Mwisa Edward alisema kuwa, wanakabiliwa na tatizo la kutokuwa na vitabu vya sheria na migogoro baina ya wafanyakazi na waajiri inayotokana na kuchelewesha stahili zao.
Alisema kuwa, kwa sasa TUGHE Kagera ina wanachama 2,285 na kuwaomba watumishi wa Serikali Kuu na Afya ambao bado hawajajiunga na chama hicho kujiunga ili kuwa na sauti ya pamoja katika kudai masilahi yao.

No comments:

Post a Comment