Na Mwandishi Wetu
SHIRIKA la Viwango nchini (TBS) limefunga kiwanda cha kutengeneza mikate
cha Yami Yami Garden Restaurant kilichopo Posta Jijini Dar es Salaam kutokana
na kutengeneza mikate bila kuwa na leseni ya viwango vya ubora wa shirika hilo.
Akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya maofisa wa shirika hilo
kufunga kiwanda hicho, Mwanasheria Mwandamizi wa TBS, Baptister Bitaho, alisema
pamoja na uongozi wa kiwanda hicho kujitetea kwamba wanaendelea na utaratibu wa
kupata cheti cha ubora cha TBS, wameamua kufunga kiwanda hicho.
"Uongozi wa kiwanda unajitetea kwamba wanaendelea na utaratibu wa
kupata cheti cha ubora, pamoja na utetezi huo, TBS imesitisha uzalishaji hadi
pale watakapopata cheti hicho kutoka kwetu," alisema.
Bitaho,
aliutaka uongozi wa kiwanda hicho kusitisha uzalishaji huku wakiwa wanaendelea
na utaratibu wa kupata kibari.
Naye, Mkaguzi
Lazaro Msasalaga, alisema kuwa shirika hilo limeamua kufanya hivyo kutokana na
mzalishaji huyo kukaidi amri ya shirika ya kumtaka afanye utaratibu wa kupata
cheti cha ubora.
Alisema zoezi
la kufungia viwanda lilianza mkoani Tanga na sasa limehamia mkoani Dar es
Salaam ambapo wanafanya ukaguzi kwenye viwanda vya mikate.
Alisema lengo
la kufanya hivyo ni kuwataka wazalishaji wa bidhaa kuthibitisha ubora kabla ya
bidhaa haijauzwa sokoni.
"Leo
tumeamua kufanya operesheni hii kuangalia kama mikate inayotengenezwa ina
viwango vya lazima na kama haikidhi hatua inayofuata ni ya kufunga
uzalishaji," alisema.
Alisema kuwa
kuna viwanda 15 tu vya kutengeneza mikate nchi nzima ambavyo vimesajiliwa na
kutokana na hali hiyo ndio maana wameamua kufanya zoezi hilo.
Kwa upande wake
Ofisa Uhusiano, Fatma Omari, alisema kuwa hawakuwa na taarifa lakini
wanaendelea na utaratibu ili waweze kufuatilia leseni ya ubora.
"Ni ghafla sana TBS kufunga
uzalishaji wa mikate, lakini tunafanya utaratibu kupata leseni," alisema.
No comments:
Post a Comment