OFISI ya Wakala wa Barabara nchini
(TANROADS ) mk o a n i Mwa n z a imekusanya sh.milioni 493.6 katika kipindi cha
mwaka mmoja uliopita kutokana na kutoza faini magari makubwa ya mizigo na
abiria ambayo yalizidisha uzito, anaripoti Wilhelm Mulinda, Mwanza.
Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mwanza,
Mhandisi Leonard Kadashi, aliliambia gazeti hili jana jijini hapa kwamba, fedha
hizo zilikusanywa kwenye mzani wa Usagara Wilayani Misungwi pamoja na Nyanguge
Wilayani Magu, kutoka Julai mwaka jana hadi Juni mwaka huu.
Mhandisi huyo alisema kuwa kati ya
magari 76,877 yaliyopimwa kwenye mizani hiyo miwili katika kipindi hicho,
magari 8,730 yalikutwa yakiwa yamezidisha uzito na hivyo kutozwa faini.
Kutokana na hali hiyo, mhandisi huyo
amewataka madereva pamoja na wamiliki wa magari makubwa ya mizigo na abiria
kufuata sheria zinazosimamia matumizi ya barabara na kuhakikisha kuwa vyombo
vyao havizidishi uzito ili kuzuia barabara zisiharibike mapema.
“Lengo la TANROADS si kutoza watu
faini, bali ni kujenga barabara na kuzisimamia na kuhakikisha kwamba sheria
zinafuatwa ili barabara ziweze kudumu kwa muda mrefu,” alisema Mhandisi
Kadashi.
Alisema kuwa ni wajibu wa kila mmoja
kutunza barabara ili ziweze kudumu kwa muda mrefu bila kuhitaji kufanyiwa
matengenezo ya mara kwa mara kwa vile serikali inatumia gharama kubwa wakati wa
kutengeneza njia hizo.
Pia alisema kuwa wenye magari makubwa
ya mizigo kupita kiasi (abnormal) wanatakiwa kuomba vibali TANROADS kabla ya
kuanza safari ili kuepuka kutozwa faini ya Dola za Kimarekani 2000.
Aidha, Mhandisi huyo amewaomba
wenye magari makubwa ya mizigo na abiria pamoja na wadau wengine wa barabara
kutoa taarifa ofisini kwake juu ya vitendo vyovyote vya kuombwa rushwa na
wafanyakazi wa TANROADS kwenye mizani ili hatua ziweze kuchukuliwa dhidi yao mara moja.
No comments:
Post a Comment