22 July 2013

SERIKALI YAHAMASISHA UCHANGIAJI MAONI KATIBA MPYA



 Na Lydia Churi, MAELEZO
SERIKALI imetoa wito kwa Watanzania kuhakikisha wanachangia ipasavyo katika kutoa maoni juu ya rasimu ya katiba iliyotolewa hivi karibuni na Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini ili Tanzania ipate katiba itakayokidhi matakwa ya wananchi. Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe aliyasema hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati akizindua Kitabu kiitwacho Mabadiliko ya Katiba na Hatima ya Tanzania kilichoandikwa na Naibu Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Tanzania, Luteni Kanali Lidwino Mgumba.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Chikawe aliitaka tume ya mabadiliko ya katiba nchini kuhakikisha inawafikia wananchi wengi na kusikiliza maoni yao juu ya rasimu ya katiba iliyotolewa na tume hiyo hivi karibuni. Alisema jukumu la tume hiyo si kutetea rasimu yao ya katiba bali ni kusikiliza wananchi wana maoni gani juu ya rasimu hiyo. Aidha, waziri huyo aliwataka wajumbe wa mabaraza ya katiba kutumia nafasi waliyonayo ili ipatikane katiba itakayowajali Watanzania wote.
Waziri Chikawe alimpongeza mtunzi wa kitabu hicho kwa kutumia katiba kuandika kwa kuwa ni suala nyeti. Aliongeza kuwa wananchi hawana budi kuandika vitabu mbalimbali vinavyohusu mila na tamaduni za kitanzania ili kuzihifadhi kwa kuwa zinatoweka. Naye Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Emmanuel Nchimbi alimpongeza mtunzi wa kitabu hicho kwani amekiandika wakati mwafaka huku akiwataka watumishi wa umma kutumia ujuzi walionao kuandika vitabu mbalimbali vitakavyoelimisha umma wa Watanzania.
Awali akizungumza kwenye uzinduzi huo, Luteni Kanali Mgumba aliwasisitiza Watanzania kusoma kitabu chake ili wapate ufahamu wa masuala ya katiba na hatimaye washiriki vizuri katika mchakato wa kupata katiba mpya. Aidha katika kuhakikisha wanafunzi wa shule za sekondari wanapata uelewa wa masuala ya katiba amegawa vitabu hivyo kwa wanafunzi waliopo kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Songea na Nachingwea.

No comments:

Post a Comment