Na Lydia Churi, MAELEZO
SERIKALI imetoa wito kwa Watanzania kuhakikisha wanachangia
ipasavyo katika kutoa maoni juu ya rasimu ya katiba iliyotolewa hivi karibuni
na Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini ili Tanzania ipate katiba itakayokidhi
matakwa ya wananchi. Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe aliyasema hayo
mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam wakati akizindua Kitabu kiitwacho
Mabadiliko ya Katiba na Hatima ya Tanzania kilichoandikwa na Naibu Kamishna
Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Tanzania, Luteni Kanali Lidwino
Mgumba.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Chikawe aliitaka tume ya
mabadiliko ya katiba nchini kuhakikisha inawafikia wananchi wengi na kusikiliza
maoni yao juu ya rasimu ya katiba iliyotolewa na tume hiyo hivi karibuni. Alisema jukumu la tume hiyo si kutetea rasimu yao ya katiba bali
ni kusikiliza wananchi wana maoni gani juu ya rasimu hiyo. Aidha, waziri huyo aliwataka wajumbe wa mabaraza ya katiba kutumia
nafasi waliyonayo ili ipatikane katiba itakayowajali Watanzania wote.
Waziri Chikawe alimpongeza mtunzi wa kitabu hicho kwa kutumia
katiba kuandika kwa kuwa ni suala nyeti. Aliongeza kuwa wananchi hawana budi
kuandika vitabu mbalimbali vinavyohusu mila na tamaduni za kitanzania ili
kuzihifadhi kwa kuwa zinatoweka. Naye Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dkt. Emmanuel Nchimbi
alimpongeza mtunzi wa kitabu hicho kwani amekiandika wakati mwafaka huku
akiwataka watumishi wa umma kutumia ujuzi walionao kuandika vitabu mbalimbali
vitakavyoelimisha umma wa Watanzania.
Awali akizungumza kwenye uzinduzi huo, Luteni Kanali Mgumba
aliwasisitiza Watanzania kusoma kitabu chake ili wapate ufahamu wa masuala ya
katiba na hatimaye washiriki vizuri katika mchakato wa kupata katiba mpya. Aidha katika kuhakikisha
wanafunzi wa shule za sekondari wanapata uelewa wa masuala ya katiba amegawa
vitabu hivyo kwa wanafunzi waliopo kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Songea na
Nachingwea.
No comments:
Post a Comment