19 July 2013

MADAKTARI BINGWA KUTOA HUDUMA BURE



 Na Hamisi Nasiri, Masasi
HOSPITALI ya Mji wa Masasi mkoani Mtwara, Mkomaindo imepokea madaktari bingwa kutoka Shirika la Kimataifa la AMREF kwa ushirikiano na Serikali kwa ajili ya kusaidia kutoa huduma ya matibabu kwa magonjwa sugu ya akina mama bure kwa kipindi cha siku nne.Akizungumza na Majira jana ofisini kwake kuhusu ujio wa madaktari hao Kaimu Mganga Mkuu wa hospitali hiyo, Dkt. George Kumwembe alisema kuwa madaktari hao bingwa kutoka Shirika la AMREF kwa kushirikiana na Serikali tayari wameshawasili katika hospitali hiyo kwa lengo la kusaidia kutoa huduma ya matibabu bure kwa magonjwa sugu ya akina mama hasa yanayohusiana na matatizo ya mfumo wa uzazi.

Alisema kuwa akina mama wengi siku hizi wamekuwa wakisumbuliwa na matatizo ya mfumo wa uzazi na kuwafanya wahangaike katika hospitali za rufaa pamoja na waganga wa kienyeji kwa gharama kubwa kutafuta matibabu ya magonjwa hayo hivyo uwepo wa madaktari hao kwa siku hizo nne kutawasaidia kupata huduma stahili na kuweza kupata ufumbuzi wa matatizo yao mbalimbali yanayowasumbua na kusababisha baadhi yao kushindwa kuzaa kabisa.
Dkt.Kumwembe alisema kuwa kuwepo kwa madaktari hao sambamba na utoaji wa huduma hiyo kutawapunguzia gharama akina mama wengi wilayani humo ya kwenda katika hospitali za rufaa ambapo huko magonjwa ya aina hiyo gharama zake zinakuwa kubwa hivyo akina mama wajitokeze kwa wingi ili kupata huduma hiyo ambayo inatolewa bure na madaktari hao.
Alisema kuwa baadhi ya magonjwa ambayo akina mama yamekuwa yakiwasumbua mara kwa mara ni pamoja na uvimbe ndani ya tumbo la uzazi na kuzipa njia ya uzazi ambapo alidai kuwa moja ya tatizo linalochangia kuwepo kwa magonjwa hayo yanayohusiana na matatizo ya mfumo wa uzazi ni pamoja na magonjwa ya kujamiiana.
"Magonjwa haya mara nyingi yanasababishwa na magonjwa ya kujamiiana hivyo mimi natoa wito kwa akina mama kuitumia fursa hii kuja hapa hospitali kwa ajili ya kupata matibabu kwa hawa madaktari badala ya wao kuendelea kukimbilia kwa waganga wa kienyeji na kwamba mara wanapokumbwa na matatizo kama haya ni bora kupata vipimo vya kitaalamu kwanza na si kutafuta mitashamba,îalisema Dkt. Kumwembe.
Kwa upande wao baadhi ya akina mama ambao walifika katika hospitali hiyo kwa ajili ya kuonana na madaktari hao walielezea juu ya furaha na waliupongeza mpango huo na kusema kuwa ujio wa madaktari hao wilayani humo kutawasaidia kufahamu matatizo yao iwapo watafanikiwa kuonana na madaktari hao na kwamba wameiomba serikali kuwa mpango huo uwe wa mara kwa mara na kulaumu kwamba siku nne zilizowekwa za utoaji huduma hiyo ni chache

No comments:

Post a Comment