Na Cornary Anthony, Mtwara
SHEHENA ya kwanza ya mabomba ya ujenzi wa bomba la
gesi imewasili mkoani Mtwara na kupokewa na viongozi mbalimbali wakiongozwa na
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, katika hali ya amani na utulivu mkubwa.
Shehena hiyo ya kwanza ya
mabomba hayo iliyowasili mkoani hapa jana ina uwezo wa kujenga bomba la umbali
wa kilomita 50. Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Waziri Pinda aliwahakikishia
wana- Mtwara kwamba mchakato mzima wa kuchakata gesi utafanyika Mtwara na
Songosongo, wilayani Kilwa. Alisema mradi wa ujenzi wa mtambo wa kuchakata gesi
utajengwa na kampuni ya CETDC ya nchini China na kwamba Serikali itatoa
zaidi ya dola bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa mtambo huo.
Alitoa mwito kwa wananchi wa Mtwara kuwa walinzi wa
bomba hilo katika maeneo yao litakakopita kwa kuiga mfano wa wenzao
wanaoishi maeneo inakopita Reli ya Kati. Waziri Pinda alisema fedha kwa ajili
ya kutekeleza mradi huo kiasi cha dola bilioni moja zimekopwa kutoka Benki ya
Exim ya China kwa mkopo wa
masharti nafuu ambapo zitarejeshwa Tanzania kwa kipindi cha miaka
miwili. "Kwa hiyo mradi huu ni wa Watanzania na sio wa China kama
wengine wanavyodhani," alisema. Aliwataka wananchi wa Mtwara kuwa na imani
na Serikali kwani kila kitu kitafanyika kwa uwazi.
Waziri Pinda alisema vijiji ambapo bomba hilo litapita watanufaika
na umeme. Mbali na kunufaika na umeme, Pinda alisema wananchi wa Mtwara kupitia
mradi huo watanufaika na huduma za maji salama, elimu na afya. Mbali na hiyo
alisema mapato ya halmashauri zote za Mkoa wa Mtwara yataongezeka. Kwa upande
wake Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Maendeleo ya Petroli
Tanzania (TPDC), Marco Mwanga, aliwataka viongozi wa Mtwara na Lindi kurudi kwa
wananchi kuwapa elimu ya kutosha kuhusiana na mradi huo bila usiri.Alisisitiza kuwa ujenzi wa mradi huo hautakuwa na
faida iwapo utatumika ubabe.
No comments:
Post a Comment