Na Alex Marwa
BUNGE
ni chombo cha kutunga sheria na pia ni mmoja wa mihimili mitatu inayounda mfumo
wa utawala kulingana na mfumo wa mgawanyo wa madaraka. Mihimili mingine ni
mahakama na serikali.Katika bunge la bajeti lililopita lilipitisha
mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka 2013/14 limemalizika hivi karibuni
mkoani Dodoma na sifa nyingi alipewa Waziri wa Fedha, Dkt.William Mgimwa, kwa
dhana ya kwamba bajeti yake imelenga kumkomboa Mtanzania wa kipato cha chini.
Hali kadhalika pongezi nyingi
zilitolewa kwa kile kilichodaiwa ya kwamba wizara yake ni sikivu kwa kukubali
kusikiliza kilio cha wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi kwa kuongeza
mgawo wa wizara mbalimbali kama vile maji, kilimo chakula na ushirika, uvuvi,
nishati na madini, habari vijana na utamaduni na michezo. Baada ya bajeti kupitishwa kwa kishindo
kinachojiri hivi sasa kinashabihiana sana na ile sheria iliyopitishwa ya fao la
kujitoa, ilivyoleta suala la sintofahamu na kusababisha bunge hilo hilo ambalo
lilipitisha sheria hiyo kupokea hoja binafsi ya Mbunge wa Kisarawe, Suleiman
Jaffo na kukubali kusitisha utekelezaji wa sheria hiyo.
Ikumbukwe awali waziri wa fedha alikuwa
amekusudia kutoza kodi ya asilimia 14.5 kutoka asilimia 12 ya hapo awali katika
huduma zote za mawasiliano ya simu hii ikiwa ni pamoja huduma ya kutuma na
kupokea pesa, ujumbe mfupi yaani sms, intaneti, milio ya simu kwa anayepigiwa,
sh.1,000 kwa mwezi kwa kila kadi ya simu na tozo la asilimia 0.5 kama gharama
ya kuhamisha fedha kutoka benki maarufu kama ‘sim banking’.Baada ya majadiliano marefu na msimamo
wa mwenyekiti na kamati yake ya bajeti kupinga tozo hiyo imekuwa na msaada
mkubwa sana hususan kwa Watanzania wa kipato cha chini waliopo maeneo ya
vijijini ambao wengi wao hawana sifa za kuhudumiwa na benki.
Lakini pia huduma hii imepanua wigo wa
huduma za kifedha vijijini na hivyo ongezeko la kodi katika huduma hii
zitaongeza gharama na hivyo kuwaumiza zaidi wananchi wa hali ya chini kwa kuwa
hawana mbadala wa huduma za kifedha.
Hata hivyo, Waziri wa Fedha
alikubaliana na maoni ya kamati ya bunge ya kutojumuisha kodi hii ya asilimia
14.5 kwenye huduma ya kutuma na kupokea fedha na kupongezwa ya kwamba wizara
yake ni sikivu na hatimaye kubakisha tozo la sh. 1,000/- kwa kila kadi ya simu
kwa mwezi na hivyo kila Mtanzania anayemiliki simu ya mkononi atalazimika
kuilipia sh. 12,000 kwa mwaka.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Mawasiliano
Tanzania (TCRA), hadi kufikia mwezi Machi, mwaka huu, Tanzania ina watumiaji wa
simu za mkononi wapatao zaidi milioni 27 ambapo kwa mujibu wa Jumuiya ya watoa
Huduma wa Simu za Mkononi Tanzania (MOAT) takriban watumiaji wanaokadiriwa
kufikia zaidi ya milioni 8 wako vijijini na matumizi yao kwa mwezi ni chini ya
sh. 1,000, na hivyo kodi hii itakuwa ni mzigo mkubwa kwao.Kutokana na idadi hii ya wateja zaidi
ya milioni 27 wanaomiliki simu za kiganjani, hii ina maana ya kwamba serikali
inatarajia kukusanya zaidi ya sh.bilioni 27, kwa mwezi na hatimaye kukusanya
zaidi ya sh. bilioni 324 kwa mwaka.Kwa mujibu wa Waziri wa Fedha mapato
yatakayopatikana kwenye kodi hii ya kadi za simu yatatumika kuchangia sekta ya
elimu.
Tofauti na nchi nyingi zilizoendelea na
zinazoendelea, wenye kipato kikubwa ndiyo walipa kodi wakubwa, hali hii ni
tofauti na Tanzania ambapo kutokana na kodi hii ya kadi ya simu, tajiri
anayetumia muda wa maongezi zaidi ya sh. 500,000 kwa mwezi na mlalahoi
anayetumia sh. 1,000 wote watatakiwa kulipa kodi sawa ya kadi zao za simu.
Kimsingi h a k u n a anayepinga
serikali kutoza kodi, bali swali la kujiuliza ni je, serikali ilifanya utafiti
wowote kabla ya kufikiria kuanzisha kodi hii?Maswali mengine ya kujiuliza ni kwamba
walengwa wa kodi hii ambao ni wananchi walishirikishwa kwa kiasi gani katika
mchakato mzima wa uanzishwaji wa kodi hii?
Je, ni wananchi wangapi
wanafahamu kuhusu kodi hii?
Mimi nadhani ni vizuri serikali
ikajenga utaratibu wa kuwashirikisha wananchi hususan katika maamuzi ambayo
yana waathiri moja kwa moja ili kuondoa manung’uniko.
Mpaka sasa hali ya sintofahamu imetanda
na cha kushangaza ni kwamba tayari wananchi wanalipa kodi ya ongezeko la
thamani (VAT) katika vocha za muda wa maongezi kwa hiyo kumuongezea mwananchi
kodi nyingine ni kutomtendea haki.
Ufafanuzi wa naibu waziri
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Fedha,
Bi. Saada Salum alisema wananchi watakuwa wakikatwa kiasi kisichopungua sh.30
kwenye muda wao wa maongezi kwa siku ili mradi ifikie sh. 1,000 kwa mwezi.
Katika kipindi cha mahojiano kuhusu
malalamiko yanayotolewa na makampuni ya simu kuwa kodi hii itamuumiza
Mtanzania, mtumiaji wa kawaida alisema wizara haiwezi kujua kwa kuwa hii kodi
ndiyo kwanza imeanzishwa na wizara haiwezi moja kwa moja kukubaliana na madai
yaliyotolewa na makampuni hayo.
Alisema kuwa ikitokea hivyo na
wakisikia kauli ya wananchi ni kwa kiasi gani wameathirika, watalazimika
kuangalia nini cha kufanya ila kwa sasa hiyo kodi ndiyo imeanzishwa.
“Hatujasikia kauli ya wananchi wenyewe
jinsi gani watakuwa wameathirika na hivi sasa ndiyo kwanza kodi hii
imeanzishwa” anasema Bi.Saada.
Aliendelea kwa kusisitiza kwamba hivi
sasa mapato hayo ni muhimu sana kwa ajili ya kusaidia bajeti ya serikali.
Kuhusu ushirikishwaji wa makampuni ya
simu wakati wa mchakato wa kuanzisha kodi hii, naibu waziri alisema kupitishwa
kwa kodi kuna michakato mirefu sana ikiwemo makongamano mbalimbali, na
uanzishwaji wa kodi hii kwa kiasi fulani ulishirikisha wadau mbalimbali.
“Inaweza kuwa isiwe kampuni ya simu
moja kwa moja lakini walishirikisha sekta binafsi na kwa kawaida kuna muundo
mbalimbali lakini mchakato huu umewashirikisha pia Mamlaka ya Mawasiliano
Tanzania (TCRA) na ikumbukwe kulikuwa na mkakati wa ‘big results now’ na hii
ilitokana na resource mobilization,” anasema.
An a s ema k uwa wa t u we n g i
walishirikishwa na inawezekana kampuni moja haikushiriki lakini nyingine
zimeshiriki au mdau mmoja hajashiriki lakini wadau wengine wameshiriki.
Anasema kwa kawaida serikali huwa
inapokea sana ushauri kabla ya kuanzisha kodi, kwa hiyo lazima kuna kampuni
mojawapo ya simu itakuwa ilishiriki katika mchakato huo.
Bi. Saada anasema kuwa iwapo wizara
itapokea malalamiko rasmi ya wananchi kupitia TCRA itayafanyia kazi kuona
athari zake ikiwamo kufanya utafiti na kuona ni jinsi gani kodi hii imeleta
athari.
“Tunaona malalamiko yamekuwa
yakiandikwa sana kwenye magazeti hata kabla ya kodi hii haijaanza iwapo wizara
itapokea malalamiko tutayafanyia kazi,” anasema.
Anasema kimsingi MOAT hawajapeleka
malalamiko rasmi zaidi ya kutoa matangazo kwenye magazeti na aliwataka wananchi
wasitaharuki kwa kuwa kodi hii itakuwa inakatwa kidogo kidogo sana hata haiwezi
kuwaathiri kwa siku nzima na huenda ikawa senti 20 au 30 kutegemeana na
matumizi ya simu ili mradi kwa siku moja iwe sh. 30.
Alifafanua ya kwamba na kodi hii haipo
kwa kadi zote za simu bali zile ambazo zitakuwa zinafanya kazi na wizara
inatambua ya kwamba wapo watumiaji wenye simu zaidi ya moja na sio zote ambazo
zitakuwa zinafanya kazi.
Anasema kuwa hana uhakika iwapo
mtumiaji atakuwa akioneshwa amekatwa kiasi gani na watumiaji ambao hawaweki
pesa wanapokea tu simu hawatatozwa kodi hii kwa kuwa makato yatakuwa
yakifanyika kupitia muda wa maongezi.
MOAT
Wakati naibu waziri akisema kuwa
mchakato wa uanzishaji wa kodi hii uliwahusisha wadau wa makampuni ya simu kwa
namna moja au nyingine, taarifa iliyotolewa katika vyombo vya habari na MOAT
imezidi kusisitiza ya kwamba haikushirikishwa katika mchakato huo.
Taarifa hiyo inasema kuwa bali
walikutana na Kamati ya Bajeti ya Bunge ili kupata usahihi wa maana ya huduma
za mawasiliano ya simu kama ilivyoainishwa katika mswada wa mwaka 2013, ambapo
mawasiliano ya simu yalitafsiriwa kuwa ni huduma yoyote inayotolewa na Kampuni
ya mawasiliano ya simu kwa kutuma, kupokea mawimbi, maneno, picha, sauti au
habari ya aina yoyote kwa kutumia mfumo wa kielektroniki wa picha au mfumo mwingine
wowote.
MOAT inaeleza kuwa inatambua jitihada
za serikali katika kukusanya kodi kwa ajili ya mipango ya maendeleo kwa
wananchi, hata hivyo imebainisha kuwa kuanzishwa kwa kodi hii kunakinzana na
juhudi za kuwapunguzia mzigo wa kodi wananchi wenye kipato cha chini.
Jumuiya hiyo inasema kuwa ukuaji wa
mawasiliano ya simu katika muongo ujao utatoka maeneo ya vijijini hivyo
uanzishwaji wa kodi hii ya sh.1,000 kwa kila mtumiaji wa simu kila mwezi
utazuia juhudi zaidi za ukuaji wa huduma ya mawasiliano katika maeneo ya
vijijini kwa sababu watu wengi ambao ni wenye kipato cha chini hawataweza
kumudu huduma ya mawasiliano.
Maoni ya wananchi
Mkazi wa Mbagala jijini Dar es Salaam,
Bw.Yohana Noah anasema anasikia tu iliongelewa bungeni kuwa wananchi wanapaswa kulipia
kadi za simu sh. 1,000 na hafahamu nini kinachoendelea ila anaamini serikali
haijatenda haki kwa kuwa maisha ni magumu,.
“Tunalipa ankara za umeme, maji na
ving’amuzi na hivi sasa hata kumiliki simu ya kiganjani imekuwa anasa, hii
inashangaza sana,” alisisitiza.
Anasema kuwa kuna vyanzo vingi vya
mapato ila anashangaa ni kwa nini watu wenye kipato cha chini wanakandamizwa.
Naye mkazi mmoja wa Gongolamboto
Mzambarauni aliyejitambulisha kwa jina Amina Said anasema hana taarifa na kodi
hiyo na hajui chochote kuhusiana na hilo, ila baada ya kufafanuliwa kuwa kuna
kodi ya sh. 1,000 kwa mwezi alisema, kodi inapaswa kuwepo kwa watu wanaofanyia
biashara simu zao na sio hata kwa wale ambao hawana biashara yoyote na simu zao
zaidi ya mawasiliano tu.
“Kodi hii ni aina nyingine ya ufisadi
na inaonesha ni jinsi gani viongozi wetu hawana huruma kwa wananchi, hata kama
wameamua kuweka kodi hii mbona hakuna uwazi ni jinsi gani itakuwa inakusanywa?”
Anasema Bw. Sebastian Sungi wa Gongolamboto.
Anasema nchi ina vyanzo vingi vya
mapato na hakukuwa na sababu ya kuanzisha kodi hii.
CCM
Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye anasema kuwa CCM inapinga tozo hii kwa
kuwa ni mzigo kwa wananchi na haikuzingatia tofauti ya vipato vya wananchi
ambao wengi wao matumizi yao ni ya kiwango cha chini.
“Kama chama tawala hatuwezi kukaa kimya
kwenye jambo ambalo tunaliona linawabebesha mzigo wananchi na huenda
likarudisha nyuma maendeleo yao na Taifa, hivyo kuchelewesha jitihada za
kuboresha maisha ya Watanzania kwa ujumla,” anasema Bw. Nape katika taarifa
yake.
Anasema kuwa cha kushangaza ni kwamba
serikali iliyopo madarakani ni ya CCM na wabunge wengi ambao siku zote tumekuwa
tukishuhudia bungeni kura zikipigwa wao huongoza kwa kusema ‘ndiyooooo...’ ni
wa CCM, na kodi hii ilipata baraka za baraza la mawaziri ambalo ni la serikali
ya CCM.
Hivyo kauli hii ya Nape imechelewa
sana.
Naye Naibu Waziri wa Mawasiliano,
Sayansi na Teknolojia, January Makamba akizungumza na gazeti hili hivi karibuni
alisema kuwa suala hili linapaswa kuangaliwa upya kwa kuwa ni nyeti na linagusa
wananchi.
Anasema kuwa anakubali kwa dhati tozo
hii itazamwe upya ili kuwapunguzia wananchi ukali wa maisha na kumtaka Mbunge
wa jimbo la Ubungo,John Mnyika kuacha kulifanya suala hili ni la kisiasa.
Hata hivyo inaonesha kuwa kauli hii ina
mkanganyiko mkubwa kwa kuwa kwa mujibu wa maelezo ya Naibu Waziri wa Fedha, Bi.
Salum, Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia ilishirikishwa katika
mchakato mzima wa kuipitisha kodi hii na hivyo inashangaza pale naibu waziri
ambaye alishiriki kubariki kodi hii, kugeuka na kusema kodi hii ni mzigo kwa
wananchi.
Kimsingi wananchi wanaeleza kuwa
serikali ilikurupuka katika hili na yeye kama ambavyo ilikurupuka kwenye sheria
ya fao la kujitoa, hivyo hivyo ni vizuri kutafutia ufumbuzi suala hili badala
ya kulikwepa na kuwepo kwa lawama na manung’uniko yaliyotokana na tozo hii.
Imefika
wakati kwa serikali kujenga utamaduni wa kufanya tafiti kwanza kabla ya
kuanzisha tozo mbalimbali na sio kus
No comments:
Post a Comment