17 July 2013

FAIDA ANWANI ZA MAKAZI ZAELEZWA


 Na Reuben Kagaruki
NAIBU Katibu Mkuu Wizara ya Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia,Prof. Patrick Makungu, amesema mpango wa utekelezaji, uanzishaji wa Anwani za Makazi na Misimbo (alama) ya posta itasaidia kurahisisha mawasiliano na kuchochea maendeleo nchini.
Profesa Makungu alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam mara baada ya kufungua semina ya siku moja ya wakurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa wizara hiyo katika kuwajengea uelewa pamoja na kuhamasisha matumizi ya anwani za makazi na misimbo ya posta.

Alisema hatua hiyo ni muhimu katika ulimwengu wa sasa katika kurahisisha mawasiliano na maendeleo.
Alibainisha kuwa jiji la Dar es Salaam ni muhimu zaidi kwa sababu huchangia asilimia 70 ya mapato yatokanayo na kodi.
Alisema awamu ya kwanza ya mpango huo kwa jiji la Dar es Salaam ilizinduliwa rasmi na Septemba 14, 2012 na Rais Jakaya Kikwete ambapo utekelezaji wake unahusisha serikali, taasisi za serikali, taasisi zisizo za kiserikali na sekta binafsi.
Profesa Makungu alisema, Mkoa wa Dar es Salaam umeanza kutekeleza mpango huu ambapo tayari baadhi ya wizara na taasisi zimeanza kutumia misimbo hiyo ya posta na wananchi wahamasike kuupokea.
Alisema, kamati tendaji kwa kushirikiana na wizara ya mawasiliano, sayansi na teknolojia na mamlaka ya mawasiliano Tanzania, Shirika la Posta, Manispaa zote za Mkoa wa Dar es Salaam na wadau mbalimbali wameandaa mipango ya utekelezaji katika jiji zima.
Naye Mkurugenzi wa Masuala ya Posta, Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania, Rehema Makubwi, alisema programu hiyo itasaidia huduma za posta kuimarika.
"Pia inasaidia katika kutambua wananchi walipo; na wakati wa dharura ya majanga kama magonjwa na moto kupata huduma kwa urahisi na huu ndiyo mfumo nzuri zaidi katika kukabili masuala haya.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Wizara ya Uchukuzi, Issa Nchasi, alisema mpango huo katika wizara yake umefika wakati mwafaka.
"Hii itaongeza ufanisi katika Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari na Maziwa (TPA), mizigo au bidhaa kumfikia mmiliki moja kwa moja bila ya kubahatisha alipo kutokana na kuwepo kwa anwani za uhakika,"alisema.

No comments:

Post a Comment