19 July 2013

BIDHAA BANDIA TANI 6 ZATEKETEZWA

Na Elizabeth Joseph,Dodoma.

 MAMLAKA ya chakula na Dawa (TFDA) imeteketeza tani 6.143 za bidhaa mbalimbali ikiwemo chakula, dawa za binadamu, mifugo pamoja na vipodozi katika kipindi cha mwaka 2012/13.Hayo yalibainishwa hivi karibuni mkoani hapa na Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Kanda ya Kati, Florent Kyombo wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari na kuongeza kuwa bidhaa hizo zilikuwa na thamani ya zaidi ya sh.milioni 92.
Kyombo alisema kuwa bidhaa hizo ziliteketezwa katika Mikoa ya Dodoma, Singida, Tabora na Kigoma ambapo katika zoezi hilo jumla ya vibali mia tatu kumi na tisa vya kuteketeza bidhaa vilitolewa kwa mwaka wa fedha wa 2012/13 ambayo ni sawa na asilimia 638 ya lengo la kuteketeza shehena 50 kwa mwaka wa fedha uliopita.Aidha Kyombo aliwataka wananchi kuwa na uelewa wa kusoma tarehe za mwisho wa matumizi ya bidhaa mbalimbali wanazonunua madukani ili kujua muda wake wa matumizi kama umemalizika.
Pia aliwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa kutoa taarifa TFDA iwapo watagundua kuwa kuna maduka yanauza bidhaa ambazo ni feki ama zimemalizika muda wake ili hatua stahiki zichukuliwe.Hata hivyo alitoa wito kwa wadau na wananchi kwa ujumla kuhakikisha wanafuata Sheria za TFDA ikiwa ni pamoja na kulipia majengo yao kwa wakati na kuwa na vibali vya kuendeshea biashara zao ili kuepuka usumbufu
.

No comments:

Post a Comment