05 February 2013

Apigwa risasi akidaiwa sh. 100 ya maji



Na Heri Shaaban

JESHI la Polisi Mkoa wa Temeke, linatarajia kumfikisha mahakamani mkazi wa Tandika, Mtaa wa Kilimahewa Bw.
Chacha Mang'ana (54), akituhumiwa kumpiga risasi jirani yake Frank Filias (25), kwa madai ya kutolipa sh. 100 ya maji.

Akizungumza na Majira Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi mkoani humo, Engelbert Kiondo, alisema tukio hilo limetokea
hivi karibuni nyumbani kwa mtuhumiwa.

Alisema chanzo cha tukio hilo ni mke mdogo wa mtuhumiwa kugombana na mama wa majeruhi Bi. Sara Mwaikatale ambaye alikuwa akidaiwa sh. 100 ambayo alichota maji.

“Mama wa majeruhi alikwenda kuchota maji nyumbani kwa mtuhumiwa Bw. Mang'ana, ambaye ana wake wawili baada,
alipofika eneo hilo alimsalimia mke mdogo ambaye hakuitikia
hivyo alichukua sh. 100 na kuiweka chini karibu na ukuta
akaondoka zake,” alisema Kamanda Kiondo.

Aliongeza kuwa, baada ya muda mke wa mtuhumiwa alimtuma mtoto wake nyumbani kwa Bi. Mwaikatale akachukue sh. 100
ambapo mama huyo alimwambia tayari alishatoa kwa kuiweka
chini karibu na ukuta wa nyumba.

Majibu hayo yalianza kuibua mzozo kati ya Bi. Mwaikatale na na mke wa Bw. Mang'ana. Ilipofika jioni mtoto wa Bi. Mwaikatale alikwenda kuchota maji ambapo bombani alimkuta mtuhumiwa
ambaye alimchapa mtoto huyo vibao.

Kutokana na hali hiyo, majeruhi aliamua kwenda nyumbani kwa mtuhumiwa kuuliza chanzo cha mtoto huyo kupigwa ndipo Bw. Mang'ana alipompiga risasi kwenye paja na nyingine aliipiga hewani.

Kamanda Kiondo alisema, polisi walifika eneo la tukio ambapo majeruhi alikimbizwa Hospitali ya Temeke na kulazwa. Kutokana
na tukio hilo, baadhi ya wananchi wenye hasira waliamua kuvamia nyumbani kwa mke mdogo wa mtuhumiwa, kumfanyia fujo na kuiba vitu mbalimbali.

No comments:

Post a Comment