31 January 2013

Twende Kanisani kuzinduliwa Febr. 10



Na Mwandishi Wetu

MSANII wa nyimbo za injili anayekuja juu nchini, Kennedy Daudi ameahidi burudani ya nguvu kweli katika uzinduzi wa video ya albamu yake ya ‘Twende Kanisani’ utakaofanyika katika Bwalo la Magereza, Ukonga Dar es Salaam Februari 10, mwaka huu.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi Dar es Salaam jana, Daudi alisema uzinduzi huo unatarajiwa kunogeshwa na wasanii wengine kibao wa nyimbo za injili.

Aliwataja wasanii watakaomsindikiza siku hiyo kuwa ni Bonny Mwaitege, Martha Mwaipaja, Emmanuel Mgaya ‘Masanja Mkandamizaji’, Frola Mbasha na kwaya mbalimbali maarufu nchini.

Baadhi ya kwaya zinazotarajiwa kuwepo ni Bethel, Shalom, Utukufu na Malaika Band zinazohudumu katika Kanisa Anglikana Parish ya Ukonga Mazizini.

“Kila kitu kipo tayari kwa ajili ya uzinduzi wa albamu hiyo na naamini watakaohudhuria, watapata kitu tofauti na watarudi wakiwa wameshiba pia ujumbe uliomo,” alisema.

Kiingilio katika uzinduzi huo utakaoanza saa 8 mchana, kitakuwa sh. 20,000 kwa viti maalumu na sh. 3,000 vya kawaida.

No comments:

Post a Comment